Maiti zinaliwa na wanyama huku wezi wakiiba majeneza Makaburi ya Langata - Wabunge

"Lazima muwe makini kama mmetumia jeneza ghali katika makaburi ya Lang’ata. Siku inayofuata mnaweza mkaupata mwili wa mpendwa wenu ukiwa nje ya kaburi kwa sababu mwizi aliiba jeneza.”

Muhtasari

• Gogo alisema katika bunge la kitaifa wakati wa kutoa hoja kuhusu mswada uliowasilishwa na mbunge wa Lang’ata Phelix Odiwuor maarufu Jalang’o.

• Mswada huo ulipigiwa upato na wabunge wengi, baadhi wakiunga mkono na kutoa wito kwa mamlaka husika kuingilia kati ili kutoa suluhisho la kudumu.

Maziara
Maziara
Image: The Star

Wabunge sasa wameibua hoja kali bungeni kwamba marehemu katika makaburi pana Zaidi jijini Nairobi, Lang’ata hawawezi tena kupata pumziko la Amani baada ya kugundulika kwamba maiti hizo zinaliwa na wanyama mwitu huku wezi wakiiba majeneza.

Kwa mujiu wa taarifa hiyo iliyochapishwa katika gazeti la The Star, wabunge walisema kwamba hili linatokana na kujaa kwa maeneo hayo ya kuwapumzisha marehemu.

“Tunazika wapendwa wetu katika makaburi yeye vina vifupi na kusababisha kunyofolewa na wanyama wa mwituni. Tamaduni za Kiafrika zinataka kwamba tuwape heshima wafu, ni jambo la kushangaza kwamba wakati tunatarajia wapendwa wetu kupumzika kwa Amani, hawapati Amani na badala yake miili yao inaliwa na wanyama,” gazeti hilo lilimnukuu mbunge wa Rangwe Lillian Gogo.

Mbunge huyo alisema kwamba maiti zingine huwa hazizikwi inavyofaa bali inarundikwa tu na kuachwa kuoza na kugeuka mizoga inayonuka chefu na hivyo kuwaathiri wanaoishi karibu.

Gogo alisema katika bunge la kitaifa wakati wa kutoa hoja kuhusu mswada uliowasilishwa na mbunge wa Lang’ata Phelix Odiwuor maarufu Jalang’o.

Katika mswada wake, Jalang’o aliwasilisha vilio na malalamishi ya wakaazi wa eneo hilo wanaosema makaburi ya Lang’ata yametengwa tangu yalipotajwa kuwa yamejaa mwaka 1998 lakini yameendelea kupokea maiti katika miaka hiyo yote.

Wanyama wa pori kutoka kwa mbuga ya wanyama ya Nairobi wanafukua maiti na kuinyofoa na hivyo kuitaka wizara ya afya na kaunti ya Nairobi kuchukua hatua madhubuti.

“Hali kama hii imepelekea kujaa kwa makaburi na hata kuzikwa mara kadhaa kwa maiti kwenye kaburi moja  lenye kina kifupi na hivyo kuifanya kuwa rahisi kwa wanyama kuifukua,” alisema.

Mswada huo ulipigiwa upato na wabunge wengi, baadhi wakiunga mkono na kutoa wito kwa mamlaka husika kuingilia kati ili kutoa suluhisho la kudumu.

“Makaburi haya kusema kweli yamejaa. Kulingana na tamaduni za Kiafrika, hatuwezi kufukua maiti ili kujenga nafasi ya kuzika maiti nyingine,” Mbunge wa Buuri, Mugambi Rundikiri alisema.

Mbunge wa Tharaka, George Murugara alisema pia kwamba kando na wanyama kufukua maiti, wezi pia wametumia fursa hiyo kuiba majeneza.

“Kama hamko makini, fisi watakula maiti kama jeneza haliko katika hali sawa, na pia lazima muwe makini kama mmetumia jeneza ghali katika makaburi ya Lang’ata. Siku inayofuata mnaweza mkaupata mwili wa mpendwa wenu ukiwa nje ya kaburi kwa sababu mwizi aliiba jeneza.”