DP Gachagua asema uchumi wa nchi umefufuka na kuimarika tangu Ruto kuwa rais

“Tumelipa pesa zote zinazodaiwa na kaunti na wabunge pia wamepokea pesa zao na huu ni uchumi wa wazi ambao uchumi sasa unarudi kwenye mkondo wake. Ni ishara ya kuimarika,” alisema.

Muhtasari

• Alitoa hakikisho kuhusu kujitolea kwa serikali kuelekea ustawi wa wazee, akibainisha kuwa usajili wa Wakenya wenye umri wa zaidi ya miaka 70 unaendelea.

Gachagua
Gachagua
Image: Facebook

Naibu Rais Rigathi Gachagua sasa anadai kwamba uchumi wa nchi ambao waliupata kama umezorota umeanza kuonesha dalili za kufufuka na kupata mwamko mpya tangu wachukue uongozi yeye na mkubwa wake rais William Ruto.

Gachagua anahisi kwamba uchumi umeimarika mara dufu tofauti na jinsi walivyoupokea mwaka jana kutoka kwa mtangulizi wao Uhuru Kenyatta ambaye wameshinda wakimlaumu kuwa mpango wake wa Handshake na kiongozi wa upinzani Raila Odinga ndio uliozorotesha uchumi wa nchi.

Akizungumza mjini Bungoma Jumapili, Gachagua alitaja kutolewa kwa serikali hivi majuzi kwa Ksh.2 milioni kwa Mfuko wa Inua Jamii ambayo inalenga makundi hatarishi kama vile mayatima na Watu Wanaoishi na Ulemavu (PLWDs), pamoja na wazee.

“Rais ameagiza Hazina kutoa pesa hizi kabla ya kitu kingine chochote. Tulipata deni la miezi 16 kutoka kwa utawala uliopita, ambao ulikuwa na shughuli nyingi na BBI hadi wakasahau ustawi wa wazee wetu. Tumeisafisha,” alisema DP.

Alitoa hakikisho kuhusu kujitolea kwa serikali kuelekea ustawi wa wazee, akibainisha kuwa usajili wa Wakenya wenye umri wa zaidi ya miaka 70 unaendelea.

Mwezi uliopita, serikali ilitoa zaidi ya Ksh.8.36 bilioni kwa ajili ya mpango huo baada ya kuchelewa. Hii ilikuwa awamu ya pili kwa miezi ya Machi, Aprili, Mei na Juni.

Kama matokeo, kila mzee alipangiwa kupokea Ksh. 8,000.

Gachagua wakati uo huo alidokeza utolewaji wa Ksh.32 bilioni mapato yanayoweza kugawiwa kwa kaunti kwa mwezi wa Julai.

“Tumelipa pesa zote zinazodaiwa na kaunti na wabunge pia wamepokea pesa zao na huu ni uchumi wa wazi ambao uchumi sasa unarudi kwenye mkondo wake. Ni ishara ya kuimarika,” alisema.

 

Alikuwa akizungumza wakati wa ibada kanisani Kanduyi, ambapo alikuwa ameandamana na Rais Ruto na Waziri Mkuu Musalia Mudavadi, miongoni mwa viongozi wengine.