Ruto, Gachagua waomboleza mtangazaji wa Capital FM Sean Cardovillis

"Ujuzi wake na maarifa mapana katika michezo mbali mbali, haswa mbio za langalanga, vitakosewa sana," DP alisema kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii.

Muhtasari

• Duru kadhaa za habari ziliripoti kwamba Cardovillis alipatikana amekufa kwenye ngazi za nyumba yake, na msafishaji kando ya Barabara ya Rhapta, Westlands.

• Sean aliheshimiwa sana kwa ufahamu wake wa kina na ujuzi wa motorsport.

Sean Cardovillis na Ruto
Sean Cardovillis na Ruto
Image: Hisani

Naibu Rais Rigathi Gachagua ameungana na viongozi ambao wameomboleza kifo cha mwanahabari mashuhuri wa michezo na mkereketwa wa michezo Sean Cardovillis.

Gachagua alisema amehuzunishwa na kifo cha ghafla cha Cardovillis, ambaye alipatikana amefariki nyumbani kwake Jumamosi asubuhi.

"Ujuzi wake na maarifa mapana katika michezo mbali mbali, haswa mbio za langalanga, vitakosewa sana," DP alisema kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii.

Alituma salamu zake za rambirambi kwa familia, marafiki, na wafanyakazi wenzake katika vyombo vya habari na udugu wa michezo kwa kupoteza.

Duru kadhaa za habari ziliripoti kwamba Cardovillis alipatikana amekufa kwenye ngazi za nyumba yake, na msafishaji kando ya Barabara ya Rhapta, Westlands.

Capital FM, ambako alifanya kazi, ilimpongeza kwenye tovuti yao ya habari www.capitalfm.co.ke.

"Tuna huzuni kubwa kutangaza kwamba ulimwengu wa michezo umepoteza mojawapo ya sauti zake za kipekee-Sean Cardovillis," kampuni hiyo ilisema.

"Mchambuzi mashuhuri wa michezo ambaye alifanya kazi hapa Capital FM alifariki asubuhi ya leo nyumbani kwake Westlands, na familia yake imearifiwa."

Sean aliheshimiwa sana kwa ufahamu wake wa kina na ujuzi wa motorsport.

Wakati wa Mashindano ya WRC Safari Rally mwaka huu huko Naivasha, alimhoji Ruto, ambaye alitamba katika mashindano ya kimataifa ya michezo.

Katika salamu za rambirambi,Ruto alisema Cardovillis alikuwa mwanahabari mahiri wa michezo ambaye athari yake itakosekana sana.

Mwakilishi wa Wanawake wa Nairobi Esther Passaris alisema alihuzunishwa sana kusikia kuhusu kifo cha Cardovillis.

Alisema Cardovillis alikuwa mtangazaji mzuri ambaye mapenzi yake kwa michezo yalikuwa ya kuambukiza.

"Maoni yake yalileta furaha kwa wasikilizaji wengi," alisema.

Passaris aliongeza kuwa Cardovillis atakosekana katika jumuiya ya michezo.