logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Jamaa apongeza kanjo kufukuza wachuuzi wa mayai, "Nairobi inataka kuwa kama Dubai"

“Nairobi inatamani kuwa Dubai ijayo na unaweza kuona aina ya uwekezaji unaofanyika Eastleigh...."

image
na Radio Jambo

Habari19 October 2023 - 10:21

Muhtasari


• Kwa mujibu wa Njohi, jiji la Nairobi ni la wafanyibiashara wa mabilioni ya mtaji wala si jiji la kufanya biashara za kuchuuza vyakula kama mayai na smokie.

• “Sakaja pia anafaa kuwalenga wasukuma na waendesha bodaboda... Nairobi ni jiji la biashara kubwa ya mamilioni,” aliongeza.

Mchuuzi wa mayai na kachumbari ahesabu hasara Kanju wakivamia.

Mwanablogu mmoja kwenye mtandao wa Facebook, Councillor Njohi ameibua dhana tofauti kuhusu mjadala unaoendelea mitandaoni wa askari wa kaunti maarufu kanjo kuwahangaisha wachuuzi wa vyakula vidogo vidogo.

Wakati wengi wameonekana kuwakosoa vikali kanjo kwa kitendo cha Jumatano cha kumhangaisha mrembo mmoja mchuuzi wa mayai, kachumbari na smokie jijini kwa kutawanya mtaji wake na kutupa toroli lake kwenye gari lao, Njohi amewatete vikali kanjo na uongozi wa gavana Sakaja.

Kwa mujibu wa Njohi, jiji la Nairobi ni la wafanyibiashara wa mabilioni ya mtaji wala si jiji la kufanya biashara za kuchuuza vyakula kama mayai na smokie.

Njohi alisema kwamba jiji la Nairobi linalenga kuwa kama jiji la Dubai katika miaka michache ijayo na ili kufanikisha ndoto hiyo, ni lazima watu wa biashara za aibu kama hao wafukuzwe kabisa kutoka jijini ili kutoa nafasi kwa wawekezaji wenye mamilioni ya mitaji.

“Nairobi inatamani kuwa Dubai ijayo na unaweza kuona aina ya uwekezaji unaofanyika Eastleigh.... Maono hayo hayana nafasi kwa wachuuzi wa vyakula vya mitaani wasio na usafi wanaouza soseji na mayai ya kuchemsha kwa toroli, ambao hata hawalipi kodi za kaunti na ushuru. Asante Sakaja kwa kuwafukuza hao macho nje ya mji,” Njohi alisema.

Mwanablogu huyo pia alimsihi gavana Sakaja kuangazia katika sekta zingine za kusafisha jiji ikiwemo kuwafukuza waendesha bodaboda na wasukuma mikokoteni kutoka jijini.

“Sakaja pia anafaa kuwalenga wasukuma na waendesha bodaboda... Nairobi ni jiji la biashara kubwa ya mamilioni,” aliongeza.

Ukatili wa kanjo.

Wakati hayo yanajiri, mwanaharakati Eric Omondi aliongoza wanamitandao kumchangishia mrembo aliyeathirika katika uvamizi huo wa kanjo.

Omondi alichangisha Zaidi ya nusu milioni ndani ya masaa 3 ya kwenda live na msichana huyo kwa jina Quinter Adhiambo ambaye mtaji wake wote ulitawanywa na kuharibiwa na Kanjo baada ya kupatikana akichuuza smokie na mayai kwa toroli lake katikati mwa jiji la Nairobi.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved