Endelea kumtegemea Mungu-Gavana Wavinya Ndeti amtia moyo Mwangaza

Gavana wa Machakos alimtaka Mwangaza kuwa thabiti na kumwamini Mungu aliyemweka katika wadhifa huo,

Muhtasari
  • Alisema watu wa Meru walimpigia kura Mwangaza kwa wingi katika uchaguzi wa 2022 kwa sababu ya upendo walionao kwake, na akasema haikuwa lazima kwa MCAs kumshtaki mara mbili.
GAVANA WA KAUNTI YA MACHAKOS WAVINYA NDETI
Image: KWA HISANI

Gavana wa Machakos Wavinya Ndeti amemtetea mwenzake wa Meru Kawira Mwangaza.

Akizungumza Jumamosi, Ndeti alisema atasimama na Mwangaza sio tu kama mwanamke mwenzake bali kwa kuzingatia ukweli kwamba alikuwa akifanya kazi nzuri katika kuboresha ustawi wa maskini huko Meru.

Alisema watu wa Meru walimpigia kura Mwangaza kwa wingi katika uchaguzi wa 2022 kwa sababu ya upendo walionao kwake, na akasema haikuwa lazima kwa MCAs kumshtaki mara mbili.

Wavinya hata hivyo alipendekeza kuwa kaunti hiyo inafaa kufutwa na wakaazi wa kaunti hiyo waruhusiwe kuwapigia kura viongozi wao tena.

“Mimi nasimama na dada yangu Kawira Mwangaza, hamuwezi impeach mtu mara mbili. Mimi kama mama nitasimama na dada yangu, na nimwambie Governor Kawira kama hawa watu wanakusumbua dissolve county, chukua signature wewe na MCA mrudi nyumbani watu wachaguane tena,” Ndeti alisema.

Gavana wa Machakos alimtaka Mwangaza kuwa thabiti na kumwamini Mungu aliyemweka katika wadhifa huo, akiongeza kuwa Bunge la Seneti lina watu wenye akili timamu ambao watatathmini suala hilo na kutoa njia bora zaidi.

“Endelea kumtegemea Mungu kama ulivyofanya siku zote dada yangu Gavana Kawira. Mungu hatakuacha kamwe. Acha akupiganie vita hivi," alisema.

"Utahesabiwa haki tena; ukweli utakuweka huru rafiki yangu. Nimesimama nawe katika maombi. Usiogope, Bwana yu pamoja nawe!"Ndeti aliongeza.

Wabunge wa Bunge la Kaunti ya Meru walimtimua Mwangaza Jumatano.