Baraza la Matajiri!-Tazama utajiri wa waliopendekezwa kuwa mawaziri katika serikali ya Ruto

Jumla ya mawaziri wateule ishirini walipigwa msasa na kamati ya uhakiki ya bunge kati ya Agosti 1 na Agosti 4.

Muhtasari

•Mteule wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Kithure Kindiki alikuwa wa kwanza kupigwa msasa na kamati kuhusu uteuzi.

•Wateule wa baraza la mawaziri wote walihitajika kutangaza thamani yao ya sasa.

ni miongoni mwa walioteuliwa kwenye baraza la mawaziri
Wycliffe Oparanya, Alfred Mutua na Hassan Joho ni miongoni mwa walioteuliwa kwenye baraza la mawaziri
Image: FACEBOOK// PARLIAMENT OF KENYA

Uhakiki wa wateule wa Baraza la Mawaziri ulianza Bungeni Alhamisi, Agosti 1, 2024.

Mteule wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Kithure Kindiki alikuwa wa kwanza kupigwa msasa na kamati kuhusu uteuzi.

Mteule huyo alifika katika Majengo ya Bunge dakika chache kabla ya saa mbili asubuhi siku ya Alhamisi. Uhakiki ulipangwa kuanza saa mbili asubuhi, hata hivyo, ulicheleweshwa na ulianza saa mbili unusu asubuhi.

Mteule wa Wizara ya Afya, Deborah Mulongo Barasa alikuwa wa pili kupigwa msasa na Kamati ya Uteuzi ya Bunge la Kitaifa.

Alice Wahome wa wizara ya ardhi alifuatwa mwendo wa saa sita adhuhuri , Migos Ogamba wa elimu akaingia saa tisa alasiri, na Soipan Tuya wa Ulinzi alifunga siku hiyo mwendo wa saa kumi na moja jioni.

Siku ya Ijumaa, Agosti 2, kamati iliwapiga msasa  Andrew Mwihia (Kilimo), Aden Duale (Mazingira), Eric Muuga (Maji), Davis Chirchir (Uchukuzi) na Margaret Ndung’u (ICT).

Mnamo Jumamosi, Agosti 3, John Mbadi (Hazina), Salim Mvurya (Biashara), Rebecca Miano (Utalii), Opiyo Wandayi (Nishati) na Kipchumba Murkomen (Michezo) walitokea mbele ya  kamati ya uhakiki.

Mnamo siku ya mwisho ya Uhakiki, Agosti 4, Hassan Joho (Madini), Alfred Mutua (Kazi), Wycliffe Oparanya (Ushirika), Justin Muturi (Utumishi wa Umma) na Stella Lang'at (Jinsia) walipigwa msasa kati ya saa mbili asubuhi na saa kumi na mbili jioni..

Wakiwa mbele ya kamati hiyo, wateule wa baraza la mawaziri, waliohudumu katika baraza la mawaziri lililovunjwa na wale ambao wameteuliwa hivi majuzi, wote walihitajika kutangaza thamani yao ya sasa.

Hii hapa orodha ya thamani halisi iliyotangazwa na wateule mbalimbali;

  • Kithure Kindiki (Usalama wa Ndani), Sh544m, kutoka Sh694m mnamo Oktoba 2022.
  • Alice Wahome (Ardhi, kazi za umma), Sh327m kutoka Sh218m mnamo Oktoba 2022.
  • Soipan Tuya (Ulinzi), Sh243.4m, kutoka Sh156m mnamo Oktoba 2022.
  • Deborah Barasa (Afya), Sh455.8m
  • Julius Ogamba (Elimu), Sh790m
  • Eric Muuga (Maji), Sh 31m.
  • Andrew Karanja Mwihia (Kilimo), Sh214m
  • Aden Duale (Mazingira), Sh980m
  • Davis Chirchir (Uchunguzi), Sh508m
  • Margaret Ndung'u (ICT), Sh93.3m
  • Rebecca Miano, (Utalii)  Sh444m
  • Opiyo Wandayi, (Nishati), Sh530m
  • Kipchumba Murkomen (Michezo), Sh620m
  • John Mbadi (Hazina), Sh390m
  • Hassan Joho (Madini), Sh2.3b
  • Alfred Mutua (Leba), Sh462m
  • Wycliffe Oparanya (Ushirika), Sh600m
  • Justin Muturi (Utumishi wa Umma), Sh801m
  • Stella Langat (Jinsia), Sh70m
  • Salim Mvurya (Biashara), Sh158m