Martha Karua ajibu baada ya Raila Odinga kumwondoa kwenye picha yake ya wasifu

Raila aliondoa picha yake na aliyekuwa mgombea mwenza wake Martha Karua kwenye kichwa cha wasifu wake wa Twitter.

Muhtasari

•Huku akijibu hatua ya Raila Odinga, Kiongozi wa Narc Kenya Martha Karua alibainisha kuwa kitendo hicho ni sawa kwake.

•"Hatua iliyokaribishwa," Karua alisema.

RAILA ODINGA NA MARTHA KARUA
Image: ANDREW KASUKU

Siku ya Jumanne, mgombea wa kiti cha mwenyekiti wa Baraza la Umoja wa Afrika, Raila Odinga, alifanya mabadiliko makubwa kwenye wasifu wake wa mitandao ya kijamii.

Raila aliondoa picha yake na aliyekuwa mgombea mwenza wake Martha Karua kwenye kichwa cha wasifu wake wa Twitter na badala yake akaweka picha ya umati wa watu wakati wa mkutano uliopita wa kisiasa.

Baadaye aliondoa hata picha hiyo ya umati wa watu na kuacha kichwa wazi kichwa cha ukurasa wake. Wakenya kwenye mitandao ya kijamii hawakukosa kuona mabadiliko hayo na wengi walichukua hatua ya kuelezea hisia zao kuhusu hilo.

Huku akijibu hatua ya mgombea urais huyo wa Azimio katika uchaguzi mkuu wa 2022, Martha Karua alibainisha kuwa kitendo hicho ni sawa kwake.

"Hatua iliyokaribishwa," Karua alisema.

Hatua ya Raila ilionekana kama uthibitisho wa kutengana kwake kabisa na aliyekuwa mgombea mwenza wake katika uchaguzi mkuu wa 2022.

Mwezi uliopita, chama cha Martha Karua, Narc Kenya, kilitoa notisi ya kujiondoa kwenye muungano wa Azimio la Umoja One Kenya.

Uamuzi huo uliwasilishwa katika barua iliyotumwa kwa katibu mkuu wa muungano huo Junet Mohammed na kaimu katibu mkuu wa Narc Kenya Asha Bashir.

"Tafadhali fahamu kuwa kukaa kwetu katika Muungano wa Azimio la Umoja One Kenya hakuwezi kudumu kutokana na maendeleo ya kisiasa yaliyopo," alisema.

“Kama NARC Kenya kwa njia ya barua hii, tunatoa notisi ya kujiondoa kwenye Muungano kama ilivyoainishwa katika kifungu cha (ma) kutoka katika Makubaliano ya Muungano. Notisi hii inaanza kutumika kuanzia tarehe ya barua hii,” aliongeza.

Karua kwenye tweet kwenye X alisema "Kukaa kwetu Azimio La Umoja One Kenya Alliance hakuwezi tena".

Mbunge huyo wa zamani wa Gichugu ameonekana kutofautiana sana na Raila Odinga katika siku za hivi majuzi haswa baada ya kiongozi huyo wa ODM kuonekana kujeng ushirikiano na serikali ya Kenya Kwanza inayoongozwa na rais William Ruto.