Wasafiri 17 wakamatwa JKIA na vyeti bandia vya Covid-19

Muhtasari

• Wasafiri wanne walifanikiwa kutoroka na wanasakwa na polisi.

• UAE imeorodhesha Kenya miongoni mwa nchi 13 ambazo visa za usafiri zimepigwa marufuku kwa sababu ya kugushi vyeti vya Covid-19.

 

Picha: Hisani
Picha: Hisani

Wasafiri 17 walikamatwa katika uwanja wa ndege wa JKIA siku ya Alhamisi baada ya kupatikana na vyeti bandia vya Covid-19.

Kukamatwa kwao kunajiri baada ya Milki za Kiarabu (UAE) kuorodhesha Kenya miongoni mwa nchi 13 ambazo visa za usafiri zimepigwa marufuku kwa sababu ya kugushi vyeti vya Covid-19.

Wasafiri wanne hata hivyo walifanikiwa kutoroka na wanasakwa na polisi.

 

UAE ilisema kwamba ilichukuwa hatua hiyo baada ya kugundua kwamba baadhi ya wasafiri kutoka Kenya walikuwa wakiwasilisha vyeti gushi vya Covid-19 wanapowasili mjini Dubai.

Nchi zingine katika orodha hiyo ni; Pakistan, Iran, Yemen, Syria, Somalia, Iraq, Turkey, Afghanistan, Syria, na Libya.

Hata hivyo ni Pakistan pekee iliyothibitisha marufuku hiyo baada ya maafisa wa serikali hiyo kutoa taarifa.

Waziri wa mambo ya nje wa Pakistan alisema kwamba marufuku hiyo haitaathiri wafsafiri ambao walikuwa tayari wamepokea visa.

Haikubainika mara moja ni aina zipi za visa zilipigwa marufuku kuambatana na agizo la UAE.

Kenya siku ya Alhamisi ilisajili maambukizi ya juu zaidi ya Covid-19 kwa siku baada ya kusajili takriban maambukizi 1,500 huku idadi ya vifo pia ikipanda marudufu.

Kufikia siku ya Alhamisi Kenya ilikuwa imesajili jumla ya maambukizi 80,102 na vifo 1,427 kutokana na Covid-19.