Shughuli ya kuhesabu kura yaanza Kiambaa

Muhtasari

• Mapema baadhi ya wafuasi wa chama cha UDA walimkabili Kiongozi wa walio wengi wa Bunge Amos Kimunya katika kituo cha kupigia kura cha Kimuga wakati wa upigaji kura.

John Njuguna Wanjiku na Kariri Njama
John Njuguna Wanjiku na Kariri Njama
Image: HISANI

Baada ya kukamilika kwa zoezi la upigaji kura katika eneo bunge la Kiambaa na lile la uakilishi wadi la Muguga shughuli za kuhesabu kura sasa zimeanza katika chaguzi hizo mbili.

Katika eneo bunge la Kiambaa upinzani mkali unatarajiwa kati ya Kariri Njama wa chama tawala cha Jubilee na John Njuguna wa UDA.Wadadisi wengi wa maswala ya kisiasa wamesema kuwa chaguzi hizo ndogo ambazo zilifanyika katika ngome ya rais Uhuru Kenyatta zitabaini umaarufu wa rais dhidi ya naibu wake William Ruto ambaye anaegemea upande chama cha UDA.

Mapema baadhi ya wafuasi wa chama cha UDA walimkabili Kiongozi wa walio wengi wa Bunge Amos Kimunya katika kituo cha kupigia kura cha Kimuga wakati wa upigaji kura.

Wafuasi hao walidai kwamba Kimunya hakuwa mpiga kura wala wakala katika uchaguzi huo mdogo na hakustahili kuwepo.

Wakati huo huo, tume ya IEBC ilikanusha madai ya kufanikisha wizi wa kura katika uchaguzi mdogo wa Kiambaa kufuatia madai yaliyotolewa na Mbunge wa Gatundu Kusini Moses Kuria.

"Gari linalozungumziwa ni gari la IEBC linalotumiwa na wafanyikazi wa Tume ambao wanatoa msaada wa kiufundi kwa mchakato wa upigaji kura. Kwa hivyo madai ya Moses Kuria ni uwongo," IEBC ilisema.

Kuria hapo awali siku Alhamisi alikuwa amechapisha kwenye mtandao wa kijamii picha za gari akidai kwamba maafisa wa IEBC walikuwa wamehepesha mitambo ya KIEMS kutumia gari hilo.