COVID 19: Wagonjwa 762 wamelazwa hospitalini, 172 wapata afueni

Muhtasari

•Mtoto wa mwezi mmoja na mkongwe wa miaka 95 ni miongoni mwa wagonjwa wapya ambao wameripotiwa na wizara ya afya hivi leo.

Waziri wa afya Mutahi Kagwe
Image: MoH

Kenya imerekodi visa 95 vipya vya wagonjwa wa COVID 19 kutoka kwa sampuli ya watu 3,334 ambao wamepimwa ndani ya kipindi cha masaa 24 ambayo yamepita.

Kufikia sasa jumla ya visa ambavyo vimewahi kuripotiwa nchini imefikia 251, 152 huku asilimia ya maambukizi kwa sasa ikiwa 2.9%.

 

Hivi leo kaunti ya Nyamira inaongoza kwa maambukizi ikiripoti visa 14, Nairobi inafuata na visa 11, Nakuru 10 huku kaunti zingine zikiwa na visa chini ya 10.

Wagonjwa 172 wameweza kupona ndani ya kipindi cha masaa 24 ambayo yamepita,  138 wakiponea nyumbani huku 34 wakipona kutoka vituo mbalimbali vya afya nchini. Kufikia sasa watu 239,730 wamewahi kupona maradhi hayo nchini.

Habari njema ni kuwa hakuna kifo chochote kilichoripotiwa leo.

Wagonjwa 762 wanaendelea kuhudumiwa hospitalini huku wengine 1788 wakiwa wanahudumiwa manyumbani. Wagonjwa 47 wamelazwa katika vyumba vya wagonjwa mahututi.

Chanjo  ya Corona

Kufikia sasa watu 3, 135, 700 wameweza kupokea angalau dozi moja ya chanjo  dhidi ya Corona huku 1, 047, 852 wakiwa wamepokea dozi zote mbili.