Polisi watatu wakamatwa kufuatia kutoweka kwa mshukiwa aliyekiri kuua watoto 12 Masten Wanjala

Inasemekana kuwa alitoweka wakati usiojulikana usiku wa Jumanne ama asubuhi ya Jumatano

Muhtasari

•Maafisa ambao walitiwa pingu ni pamoja na naibu kamanda wa kituo cha polisi cha Jogoo na maafisa wengine wawili ambao walikuwa wameshika zamu.

•Takriban watu 20 ikiwemo washukiwa waliokuwa wamezuiliwa pamoja na Wanjala na baadhi ya maafia walihojiwa kuhusiana na kutoweka kwa mshukiwa.

Mshukiwa Masten Milimu Wanjala
Image: DCI

Maafisa watatu wa polisi walikamatwa  na kuzuiliwa siku ya Jumatano kufuatia kutoweka kwa mshukiwa wa mauaji ya watoto  Masten Wanjala.

Maafisa ambao walitiwa pingu ni pamoja na naibu kamanda wa kituo cha polisi cha Jogoo na maafisa wengine wawili ambao walikuwa wameshika zamu.

Kuna uwezekano wa maafisa hao kufikishwa mahakamani siku ya Alhamisi na kushtakiwa kwa kosa la kufanikisha kutoweka kwa mshukiwa na  kutowajibika kazini.

Watatu hao walikamatwa wakiwa katika maeneo yao ya kazi na kupelekwa mahali ambapo walishirikishwa kwenye mahojiano kabla ya kuzuiliwa katika kituo cha Capitol Hill wakisubiri kufikishwa mahakamani.

Takriban watu 20 ikiwemo washukiwa waliokuwa wamezuiliwa pamoja na Wanjala na baadhi ya maafia walihojiwa kuhusiana na kutoroka kwa mshukiwa.

Juhudi za kusaka mshukiwa ziling'oa nang'a baada yake kutoroka kutoka kituo cha polisi cha Jogoo katika hali tatanishi.

Iliripotiwa kuwa mshukiwa alikuwa anatarajiwa mahakamani kuhudhuria kesi dhidi yake wakati tukio hilo lilitokea.

Maafisa ambao walikuwa katika zamu waligundua kuwa Wanjala hakuwepo mida ya saa moja asubuhi wakati walikuwa wanaita majina ya washukiwa waliokuwa wamezuiliwa.

Inasemekana kuwa alitoroka wakati usiojulikana usiku wa Jumanne ama asubuhi ya Jumatano. 

Wanjala bado hakuwa amesomewa mashtaka dhidi yake.

Polisi walisema kuwa kufikia sasa mshukiwa amehusishwa na mauaji 14 katika maeneo ya Nairobi, Machakos na Magharibi mwa nchi.

Mshukiwa alikuwa amekiri kuua watoto 12 alipokamatwa mnamo mwezi Julai mwakani. Alisema kuwa aliteka nyara watoto 12 na kuwaua katika kaunti ya Nairobi, Machakos na Bungoma ndani ya kipindi cha miaka minne.

Kufikia sasa miili 5 imepatikana.

Inasemekana kuwa Wanjala alijifanya mkufunzi wa kandanda na kudanganya wahasiriwa wake kabla ya kuwaua na kutupa miili yao katika sehemu mbalimbzli za nchi.

Alikamatwa mnamo mwezi Julai alipokuwa anajaribu kudai pesa kutoka kwa wazazi wa mtoto ambaye anadaiwa kuteka nyara na kuua.

(Utafiri: Samuel Maina}