•Moto huo ambao ulizuka mwendo wa saa moja alasiri uliteketeza nguo, vitanda, masanduku kadhaa na paa ya bweni kabla ya kudhibitiwa.
•Bweni lililoteketea lilikamilika mwaka jana kwa ufadhili wa CDF kufuatia ahadi ya naibu rais William Ruto alipokuwa ametembea pale miaka miwili iliyopita.
Wanafunzi katika shule ya upili ya wavulana ya Kaheti, kaunti ya Nyeri wanahesabu hasara baada ya moto mkubwa kuteketeza bweni moja asubuhi ya Alhamisi.
Moto huo ambao ulizuka mwendo wa saa moja alasiri uliteketeza nguo, vitanda, masanduku kadhaa na paa ya bweni kabla ya kudhibitiwa. Hata hivyo hakuna yeyote aliyeumia wakati wa mkasa ule.
Wanafunzi na majirani waliofika shuleni humo punde baada ya kuona moshi mkubwa ukitokea walishirikiana kujaribu kuudhibiti moto ule kwa kutumia maji kabla haujaenea kwingine.
Moto huo tayari ulikuwa umethibitiwa wakati wazima moto kutoka eneo bunge jirani la Mathira waliwasili. Vitu kadhaa viliweza kuokolewa.
Kulingana na mashahidi, moto huo ulizuka muda mfupi tu baada ya wanafunzi kupata kiamsha kinywa na kuelekea madarasani.
Mabweni yote tayari yalikuwa yamefungwa wakati moshi mkubwa ulianza kuonekana ukitokea kwenye paa ya bweni hilo lililo karibu na madarasa.
Bweni lililoteketea lilikamilika mwaka jana kwa ufadhili wa CDF kufuatia ahadi ya naibu rais William Ruto alipokuwa ametembea pale miaka miwili iliyopita.
Haya yanajiri huku visa vya uchomaji wa shule vikiwa vimekithiri kote nchini.
Inaripotiwa zaidi ya shule 20 zimeripoti visa vya moto katika kipindi cha miezi miwili iliyopita.
Wiki iliyopita waziri wa masomo George Magoha alitangaza wazazi watagharamia hasara zote ambazo zitapatikana kutokana na matukio yale.