Mtoto wa mwaka mmoja aliyekuwa ameibiwa aokolewa baada ya msako wa siku tatu

Muhtasari

• Zawadi anadaiwa kuibiwa kutoka kwa mlango wa nyumba yao wakati kijakazi aliyekuwa ameachiwa jukumu la kumchunga alikuwa anafua nguo.

• Mama ya mhasiriwa, Anne Nanjumbia alijawa na machozi ya furaha alipompokea tena bintiye mikononi kutoka afisa wa polisi baada ya kumkosa kwa siku tat

Mtoto wa mwaka mmoja aliyekuwa ameibwa katika kaunti ndogo ya Funyula, kaunti ya Busia amepatikana baada ya siku tatu za kumtafuta. 

Maafisa wa ujasusi katika kaunti hiyo wamemtia mbaroni  mwanamke mmoja anayetuhumiwa kuiba mtoto huyo wa kike mnamo Novemba 16.

Kulingana na idara ya DCI, Electine Obonyo alikamatwa  katika eneo la Mabatini Alhamisi jioni na kuzuiliwa katika kituo cha polisi cha  Bumala baada ya kuhusishwa na wizi wa mtoto kwa jina Zawadi.

Zawadi anadaiwa kuibwa kutoka kwa mlango wa nyumba yao wakati mfanyikazi wa nyumbani aliyekuwa ameachiwa jukumu la kumchunga alikuwa anafua nguo.

Ripoti kuhusu kupotea kwa mtoto huyo ilisajiliwa katika kituo cha polisi cha Funyula na juhudi za kumtafuta zikang'oa nanga.

Iliwachukua wapelelezi siku tatu kumtafuta mtoto huyo na kwa neema zake Mola juhudi zao zikazaa matunda usiku wa Alhamisi ambapo Zawadi alipatikana akiwa buheri wa afya.

Mamake, Anne Nanjumbia alijawa na machozi ya furaha alipompokea Zawadi wake akiwa buheri wa afya kutoka kwa afisa wa polisi baada ya kumkosa kwa siku tatu.

Mshukiwa atafikishwa mahakamani kujibu mashtaka ya wizi wa mtoto.

MHARIRI: DAVIS OJIAMBO