logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Jinsi juhudi za wafungwa wa kigaidi za kuwasiliana na washirika wao baada ya kutoroka Kamiti zilidhalilishwa

Wapelelezi wa DCI wa kupambana na ugaidi wamebaini kwamba washukiwa walipofika katika mji wa Machakos walioga, wakapata kiamsha kinywa na wakanunua kofia tatu ili waweze kuficha nyuso zao wanapoendelea na safari.

image
na Radio Jambo

Habari23 November 2021 - 02:13

Muhtasari


•Washukiwa walipofika katika mji wa Machakos walioga, wakapata kiamsha kinywa na wakanunua kofia tatu ili waweze kuficha nyuso zao wanapoendelea na safari.

•Mipango yao ilidhalilishwa wakati muuza duka ambaye waliendea awasaidie kuandikisha laini za simu alisita huku akidai watoe vitambulisho

Musharraf Abdalla, Joseph Juma na Mohammed Abdi wakamatwa wakielekea Somalia

Polisi wangali wanaendelea na uchunguzi  kuhusiana na tukio la wafungwa watatu wa kigaidi kutoroka kutoka jela ya Kamiti mnamo Novemba 15.

Kulingana na taarifa ambayo  ilitolewa na DCI usiku wa  Jumanne, uchunguzi wa awali umebaini washukiwa walipofanikiwa kutoka nje ya kuta za jela walijaribu kuwasiliana na washirika wao wa ugaidi wasiojulikana walipo.

Wapelelezi wa kupambana na ugaidi wamebaini kwamba washukiwa walipofika katika mji wa Machakos walioga, wakapata kiamsha kinywa na wakanunua kofia tatu ili waweze kuficha nyuso zao wanapoendelea na safari.

Baada ya matayarisho hayo washukiwa walinunua simu mbili ambazo walikusudia kutumia kuwasiliana na wenzao.

Hata hivyo mipango yao ilidhalilishwa wakati muuza duka ambaye waliendea awasaidie kuandikisha laini za simu alisita huku akidai watoe vitambulisho.

Imebainika washukiwa hata walijaribu kumhonga muuza duka huyo ili awasaidie kupata laini ila akasimama kidete na kukaidi ombi lao.

Katika taarifa hiyo iliyochapishwa kwenye mitandao ya kijamii , DCI wamemsherehekea sana muuza duka huyo kwa kuweka nchi yake mbele badala ya pesa ambazo angefaidika nazo iwapo angekubali hongo ya washukiwa na awasaidie kuandikisha laini.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved