logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Mwanamume apatikana na hatia ya kumnajisi msichana Loitoktok

mahakama iliamua kwamba upande wa mashtaka ulithibitisha madai dhidi ya mshukiwa.

image
na

Habari02 December 2021 - 11:17

Muhtasari


• Mwanamume mwenye umri wa miaka 28 amepatikana na hatia ya kumnajisi msichana wa miaka 17 na mahakama ya Loitoktok.   

• Msichana huyo aliondoka nyumbani kwao bila kuwajulisha wazazi wake na kwenda nyumbani kwa mshtakiwa ambapo alikaa kwa siku nne. 

• Mahakama iliambiwa kwamba msichana huyo alituma ujumbe mfupi kwa mamake kwa kutumia simu ya mshtakiwa akimjulisha kuwa alikuwa na mshtakiwa. 

Mahakama

Mwanamume mwenye umri wa miaka 28 amepatikana na hatia ya kumnajisi msichana wa miaka 17 na mahakama ya Loitoktok.            

Benjamin Mutuku ambaye alifikishwa mbele ya Hakimu Mkazi, Caroline Ndumia alishtakiwa kuwa tarehe tofauti kati ya Januari 4 hadi 7, 2020 katika eneo la Olchoro huko Loitoktok alimnajisi msichana huyo. 

Msichana huyo hapo awali aliambia mahakama jinsi mnamo Januari 3, alikutana na mshtakiwa ambaye alikuwa akimfahamu kwa muda mrefu na kumwomba aende kuishi naye kama mke wake. 

Msichana huyo aliondoka nyumbani kwao bila kuwajulisha wazazi wake na kwenda nyumbani kwa mshtakiwa ambapo alikaa kwa siku nne. 

Mahakama ilisikia kwamba babake msichana huyo, Kennedy Suryanag, aliripoti katika kituo cha polisi cha Kimana kwamba bintiye alitoweka alipokosa kufika siku moja baada ya kutoweka kwake.

Mahakama iliambiwa kwamba msichana huyo alituma ujumbe mfupi kwa mamake kwa kutumia simu ya mshtakiwa akimjulisha kuwa alikuwa na mshtakiwa. 

Maafisa wa polisi walifuatilia simu ya mshtakiwa hadi nyumbani kwake ambapo waliwapata wawili hao. 

Mshtakiwa alikamatwa na kupelekwa katika Kituo cha Polisi cha Olchoro ambako alishtakiwa kwa kosa hilo huku msichana huyo akipelekwa katika hospitali ndogo ya Loitoktok ambapo ilithibitishwa alikuwa amenajisiwa. 

Katika utetezi wake mshtakiwa alikana kumnajisi mtoto huyo na kuongeza kuwa alikuwa hajawahi kumuona.

Aliambia mahakama kuwa alikamatwa akiwa anafanya biashara ya uchuuzi na kupelekwa hadi kituo cha polisi na kufunguliwa mashtaka ya unajisi. 

Hata hivyo, mahakama iliamua kwamba upande wa mashtaka ulithibitisha madai dhidi ya mshukiwa.  Atahukumiwa Desemba 6, 2021.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved