logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Wateketezaji washambulia tena na kuchoma nyumba ya mwanamke mkongwe aliyeuawa kwa madai ya uchawi Kisii

Naibu kamishna wa kaunti Patrick Muriira alisema hakuna aliyejeruhiwa katika tukio hilo la moto ila mali yenye thamani isiyojulikana  iliharibiwa.

image
na Radio Jambo

Habari07 December 2021 - 03:02

Muhtasari


•Nyumba ya Jemima Mironga ilikuwa imechomwa tena mwezi uliopita na baadae ikafanyiwa ukarabati kupitia usaidizi wa wanaharati wa kutetea haki za binadamu katika kaunti hiyo.

•Naibu kamishna wa kaunti Patrick Muriira alisema hakuna aliyejeruhiwa katika tukio hilo la moto ila mali yenye thamani isiyojulikana  iliharibiwa.

Moto mkubwa

Watu wasiojulikana wameteketeza nyumba ya mmoja wa wanawake wakongwe ambaye aliuawa kufuatia madai ya uchawi katika eneo la Kitutu Chache Kaskazini, kaunti ya Kisii zaidi ya mwezi mmoja uliopita.

Nyumba ya Jemima Mironga ilikuwa imechomwa tena mwezi uliopita na baadae ikafanyiwa ukarabati kupitia usaidizi wa wanaharati wa kutetea haki za binadamu katika kaunti hiyo.

Wanaharakati hao pia walikuwa wamejengea watoto wa Mironga nyumba ingine moja pale.

Kufikia jioni ya Jumatatu police katika eneo la Rioma bado hawakuwa wamebaini kilichopelekea uchomaji ule.

Naibu kamishna wa kaunti Patrick Muriira alisema hakuna aliyejeruhiwa katika tukio hilo la moto ila mali yenye thamani isiyojulikana  iliharibiwa.

Janet Moraa ambaye ni binti wa marehemu Mironga alisema waligundua moto huo mwendo wa saa tano usiku ila juhudi za kuuzima zikagonga mwamba kwani ulikuwa unaenea haraka.

"Tulikuwa tumelala tayari ila kwa neema yake Mungu tulinusurika kifo" Moraa alisema.

Uteketezaji huo unaonekana kuhusiana na tukio la mwezi jana ambapo wanawake wanne wakongwe ikiwemo Mironga waliuawa kwa madai ya kuteka nyara mwanafunzi wa shule ya upili usiku.

Mwanafunzi huyo alipatikana akiwa amezuzua nje ya nyumba yake asubuhi iliyofuata.

Moraa aliomba ulinzi kutoka kwa serikali kufuatia tukio hilo huku akidai maisha ya familia yao yalikuwa hatarini.

Muriira alisema polisi wameanzisha uchunguzi.

(Utafsiri: Samuel Maina)


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved