Waziri wa Elimu George Magoha, Jumatatu akikagua ujenzi wa madarasa katika kaunti ya Mombasa aliwaonya walimu wakuu dhidi ya kufukuza wanafunzi ambao hawajalipa karo.
Magoha aliwataka walimu wakuu kuwa makini na wanafunzi wakorofi kabla ya mitihani ya KCPE na KCSE, alifichua kuwa wizara tayari imetoa pesa kwa shule kabla ya kufunguliwa kwa kwa muhula wa tatu mnamo Januari 4, 2022.
Magoha alisisitiza kwamba hakuna mwalimu ambaye ana haki ya kumnyima mwanafunzi masomo kwa kukosa kulipa karo ya shule
"Hakuna mtoto Mkenya anayepaswa kuwa nje ya shule kwa sababu ya karo katika mwaka mpya, serikali itahakikisha kwamba pesa zinapatikana kufikia Januari," Waziri alisema
Alieleza kwamba wamekubaliana na walimu wakuu wakubali kidogo ambacho wazazi watapeleka shuleni kulingana na uwezo wao.
"Kama mzazi hataki mtoto aende shule mwache amweke nyumbani. Maana tumewaambia wakuu kwamba ikiwa ni kesi ya kweli basi wachukue kile ambacho mzazi amemleta shuleni na wakubaliane jinsi ambavyo vingine vitalipwa,”
Magoha alisema watoto ambao wamehusishwa na visa vya kuchoma shule hawataruhusiwa kurejea humo, na kusema wahusika walio katika kidato cha nne itawalizimu kufanya mitihani wakitoka nyumbani kwao
"Watoto waasi wanaotaka kwenda nyumbani kupumzika, tutawaruhusu. Ikiwa kuna mtoto hataki kwenda shule na anataka kwenda kupumzika na wazazi wake, kufanya mitihani kutoka nyumbani, aende, badala ya kuharibu rasilimali, kwa sababu ni ujinga.kwa sababu anataka kila mtu ateseke kwa hivyo mnachoma shule na kila mtu anateseka tutakuwa waangalifu sana,” Magoha alisema