Ruto adai hatua sawa za kisheria kuchukuliwa dhidi ya wachochezi wote bila ubaguzi

Muhtasari

•Ruto alisisitiza kwamba chama chake cha UDA ni cha kidemokrasia na kinalenga kuangazia masuala muhimu wala sio ukabila.

•Haya yanajiri siku chache tu baada ya seneta wa Meru Mithika Linturi kutoa matamshi yaliyodaiwa kuwa ya kichochezi katika mkutano wa Ruto uliofanyika Eldoret.

Naibu rais William Ruto
Naibu rais William Ruto
Image: MAKTABA

Naibu rais William Ruto ametoa wito kwa hatua sawa za kisheria kuchukuliwa dhidi ya wachochezi wote bila kujali mwelekeo wao wa kisiasa.

Alipokuwa anahutubia wananchi mjini Bomet siku ya Jumatatu Ruto alisema hatua hiyo itasaidia katika kufanikisha usalama wa nchi.

Ruto alisisitiza kwamba chama chake cha UDA ni cha kidemokrasia na kinalenga kuangazia masuala muhimu wala sio ukabila.

"Tunataka sheria sawa itumike kwa kila mchochezi nchini Kenya, iwe ni wa UDA au kutoka upande huo mwingine ili tuweke nchi yetu salama. Sisi ni chama cha kidemokrasia na tunaamini kila mtu ako huru kuchagua upande ambao anataka kuwa, yule ambaye anataka kuchagua na chama ambacho anataka kujihusisha nacho. Sisi ni wademokrasia na tuko tayari kushindana kuhusu masuala sio ukabila, jukwaa la ajenda wala sio kuangazia sekta fulani za jamii" Ruto alisema.

Naibu rais alisema chama chake kimejumuisha viongozi wengi kutoka maeneo mbalimbali ya Kenya. Alidai kwamba chama chake kitaleta mabadiliko yanayohitajika nchini.

Haya yanajiri siku chache tu baada ya seneta wa Meru Mithika Linturi kutoa matamshi yaliyodaiwa kuwa ya kichochezi katika mkutano wa Ruto uliofanyika Eldoret.

Mwandani huyo wa naibu rais alipokuwa anatoa hotuba yake alitoa matamshi 'kuondoa madoadoa' ambayo yamekosolewa sana na hata kupelekea kukamatwa kwake.

"Sisi tunataka kuwa kwa serikali inayokuja lakini nawaambia watu wa Uasin Gishu msicheze na Kenya na kile nawaomba ni kwamba madoadoa yale mliyonayo hapa muweze kuondoa. Hatuwezi kuwa tukisimama na William Ruto kule Mt Kenya na mko na wengine hapa hawasikii na hawawezi ungana naye..." Linturi alisema.

Seneta huyo alikamatwa asubuhi ya Jumapili katika hoteli moja mjini Eldoret na kusafirishwa hadi jijini Nairobi.