"Nimevunjika lakini sijaharibiwa!" Itumbi azungumza kuhusu afya yake

Muhtasari

•Itumbi amesema kwa sasa ana sababu za kufurahi kwani angali anaendelea kupona na ana matumaini makubwa ya kupata afueni. 

•Mwanablogu huyo aliyezingirwa na utata mwingi amewasuta maafisa wa polisi ambao alidai walimtesa huku akisisitiza kwamba bado hatishiki licha ya yote.

Mwanablogu Dennis Itumbi aliruhusiwa kutoka hospitalini
Mwanablogu Dennis Itumbi aliruhusiwa kutoka hospitalini
Image: HANDOUT

Mwanablogu Dennis Itumbi hatimaye ametoa taarifa kuhusu afya yake kwa sasa takriban wiki moja baada ya kupewa ruhusa kutoka hospitalini.

Kupitia ukurasa wake wa Facebook, Itumbi amesema kwa sasa ana sababu za kufurahi kwani angali anaendelea kupona na ana matumaini makubwa ya kupata afueni. 

Mtaalamu huyo wa masuala ya kidijitali wa Ruto amewashukuru wote waliomuombea, wakamtia moyo na kumtakia mema alipokuwa anaugua.

"Nilikuwa na sababu ndogo sana za kusema, "Krismasi Njema", lakini nina kila sababu ya kufurahi, "Heri ya Mwaka Mpya". Hakika, Mungu hufanya kazi kwa njia zisizoeleweka, na ukombozi wangu, uponyaji unaoendelea na tumaini la kesho iliyo bora ni ushuhuda wangu wa neema tele. Asanteni kwa maombi yenu yasiyokoma, kunitakia mema na kunitia moyo. Nia yenu  njema ilinisaidia kupita katika hali mbaya zaidi na kurejesha imani yangu katika wema wa watu" Itumbi amesema.

Mwanablogu huyo aliyezingirwa na utata mwingi amewasuta maafisa wa polisi ambao alidai walimtesa huku akisisitiza kwamba bado hatishiki licha ya yote.

Nimevunjika, lakini sijaharibiwa. Nina nguvu na jamani, nimepumzika! mmetusaidia kufikia hatua inayofuata! Yaja.." Ameandika.

Amesema kwamba kutakuwa na ibada ya kumshukuru Mungu kwa aliyomtendea mnamo Februari 13 katika eneo bunge alilotoka la Gichugu.