Jamaa aua kakake mkubwa kwa panga juu ya deni la Ksh 10 ,Kapsabet

Muhtasari

•Mama yao alifika katika eneo la vita kuchelewa kwani tayari mwanawe mdogo alikuwa amechukua panga na kuitumia kukata mkubwa wake usoni na kumwacha akivuja damu nyingi.

Crime scene
Crime scene
Image: HISANI

Jamaa mmoja mwenye umri wa miaka 31 alipoteza maisha yake kutokana na jeraha baya la panga alilosababishwa na mdogo wake Ijumaa asubuhi katika kijiji cha Kaminon, kaunti ya Nandi

Marehemu na kakake mdogo Brian Mwale Ilondaga 28, ambao wamekuwa wakiishi katika kiwanja kimoja walivurugana kwa mangumi na mateke mwendo wa saa kumi na mbili alfajiri wakizozana  kuhusu deni la Sh10 alilokuwa anadaiwa mmoja wao.

Mvurugano huo ulifurusha mama yao kutoka usingizini kisha akaelekea walikokuwa wanapimania nguvu ili kujaribu kuwatenganisha.

Ajuza huyo alifika katika eneo la vita kuchelewa kwani tayari mwanawe mdogo alikuwa amechukua panga na kuitumia kukata mkubwa wake usoni na kumwacha akivuja damu nyingi.

Kuona hayo alipiga nduru na kuita majirani ambao walimkimbiza mhasiriwa katika hospitali ya rufaa ya Kapsabet ili kupokea matibabu ya dharura ila akapoteza maisha yake.

Mshukiwa alikamatwa na kuzuiliwa katika kituo cha polisi cha Kaimosi akisubiri kufikishwa mahakamani Jumatatu.