ODM yakana madai kuwa viongozi wake walimpendekeza Khalwale kuwa gavana wa Kakamega

Muhtasari

•ODM ilisema madai ya  awali ya Khalwale kuwa alikutana na viongozi wa chama hicho kutoka eneo la Ikolomani ni ya uongo.

•Khalwale pia alidai kuwa mwenyekiti wa chama hicho katika eneo bunge la Ikolomani Bw Vincent Mukhono alijiunga rasmi na UDA.

Seneta wa zamani wa Kakamega Boni Khalwale
Seneta wa zamani wa Kakamega Boni Khalwale
Image: MAKTABA

Chama cha ODM  kimepuuzilia mbali madai kwamba maafisa wake walishiriki kikao na seneta wa zamani wa Kakamega Bonny Khalwale na kumpendekeza kuwa gavana ajaye wa kaunti hiyo.

Katika taarifa iliyotolewa Jumatatu, ODM ilisema madai ya  awali ya Khalwale kuwa alikutana na viongozi wa chama hicho kutoka eneo la Ikolomani ni ya uongo.

Chama hicho ambacho kinaongozwa na waziri mkuu wa zamani Raila Odinga kimesisitiza kwamba hakuna afisa yeyote kutoka kaunti ya Kakamega aliyekutana na mwandani huyo wa naibu rais William Ruto wala kumpendekeza kuwa gavana.

"Hakujawa na mkutano wowote kati ya viongozi wa ODM na aliyekuwa Seneta wa Kaunti ya Kakamega Dkt Bonny Khalwale. Hakuna afisa wetu hata mmoja katika kaunti ya Kakamega ambaye amekutana naye na kumpendekeza kama anavyodai kwenye ukurasa wake wa Twitter. Hao ni wadanganyifu." Ujumbe wa ODM ulisoma.

Hapo awali mgombeaji huyo wa kiti cha Ugavana cha Kakamega alidai kwamba alikutana na viongozi mbalimbali kutoka kaunti hiyo ikiwemo wale wa ODM na wakampendekeza kurithi kiti kitakachoachwa wazi na gavana wa sasa Wycliffe Oparanya.

Khalwale pia alidai kuwa mwenyekiti wa chama hicho katika eneo bunge la Ikolomani Bw Vincent Mukhono alijiunga rasmi na UDA.

"Kando na kupendekezwa huko, mwenyekiti wa ODM katika eneo bunge la Ikolomani Bw Vincent Mukhono amehamia chama cha UDA na atawania kiti cha ubunge cha Ikolomani" Khalwale alisema.

Mbunge huyo wa zamani wa Ikolomani atakuwa anajaribu bahati yake katika kinyang'anyiro cha ugavana wa Kakamega kwa mara ya pili mwaka huu.