Kizaazaa bungeni, jamaa ajitokeza akilia akisema ni mjukuu wa hayati Kibaki

Muhtasari

• Jamaa mmoja amejitokeza katika majengo ya bunge huku akilia kwa sauti ya juu akimuomboleza hayati rais Mwai Kibaki.

• “Mbona ulienda mapema hivi,” alisema huku akibubujikwa na machozi.

• Juhudi za maafisa wa polisi kumtuliza ili aruhusiwe kuingia ndani ya malango ya bunge kuutazama mwili wa Kibaki ziliambulia patupu.

Jamaa mmoja amejitokeza katika majengo ya bunge huku akilia kwa sauti ya juu akimuomboleza hayati rais Mwai Kibaki.

Mwanamume huyo ambaye alifika katika majengo ya bunge siku ya Jumanne  alidai kuwa mjukuu wa marehmu Kibaki.

“Mbona ulienda mapema hivi,” alisema huku akibubujikwa na machozi.

Jamaa huyo alisema kifo cha rais mustaafu Mwai Kibaki kilimuathiri sana.

Juhudi za maafisa wa polisi kumtuliza ili aruhusiwe kuingia ndani ya malango ya bunge kuutazama mwili wa Kibaki ziliambulia patupu.

“Mniruhusu nimuone kwa mara ya mwisho,” aliambia maafisa wa polisi.

Maafisa wa polisi baadaye walilazimika kumuondoa kutoka majengo ya bunge baada ya juhudi za kumtuliza kugonga mwamba

Hata alivua baadhi ya mavazi yake, kupinga hatua ya kuondolewa kutoka majengo ya bunge kumzuia kumuona ‘babu yake’.

Mwili wa rais Mustaafu Mwai Kibaki uliwasili katika majengo ya bunge Jumanne asubuhi kwa siku ya pili ya hafla ya mwili huo kutazamwa na wananchi.