Mshukiwa wa nne wa mauaji ya mwanafunzi wa KIMC akamatwa, ushahidi muhimu wapatikana

Muhtasari

•Jumatatu asubuhi polisi walimtia mbaroni mshukiwa wa nne Isaac Kariuki Kibui, 22, katika baa ya Thindigua Delish Nail.

•Mwili wa Wangechi ulipatikana Jumamosi asubuhi  kando ya barabara iliyo karibu na mtaa wa Mburiria, Kaunti ya Kiambu. 

Mshukiwa wa nne Isaac Kariuki na marehemu Purity Wangechi
Mshukiwa wa nne Isaac Kariuki na marehemu Purity Wangechi
Image: TWITTER// DCI

Polisi katika kaunti ya Kiambu wameendelea kuwasaka washukiwa zaidi wa mauaji ya Purity Wangechi ,19, ambaye alikuwa mwanafunzi katika  Kenya Institute of Mass Communication (KIMC).

Jumatatu asubuhi polisi walimtia mbaroni mshukiwa wa nne Isaac Kariuki Kibui, 22, katika baa ya Thindigua Delish Nail.

Kariuki alisindikizwa hadi nyumbani kwake na maafisa waliomkamata ambako ushahidi muhimu ulipatikana.

Polisi waliweza kupata koti lililokuwa na damu nyumbani kwa mshukiwa. Inaaminika kuwa mshukiwa alikuwa amevalia koti hilo usiku ambao Wangechi aliuawa.

Kitengo cha DCI kimeripoti kuwa koti la Kariuki litafanyiwa uchambuzi wa kitaalamu katika maabara yao. Wataalamu wa DNA wanatarajiwa kubaini ikiwa madoa ya damuyaliyopatikana kwenye koti la mshukiwa yanalingana na sampuli za damu ya marehemu.

Mwili wa Wangechi ulipatikana Jumamosi asubuhi  kando ya barabara iliyo karibu na mtaa wa Mburiria, Kaunti ya Kiambu. Mwili wa marehemu ulikuwa na majeraha ya kisu na ishara za kunyongwa.

Uchunguzi wa polisi umebaini kuwa Wangechi aliuawa alipomkabili  mpenzi wake John Wanyoike Kibungi almaarufu VDJ Flexx, baada ya kugundua kuwa yeye ni jamaa hatari.

Flexx ambaye anaaminika kuwa mpangaji mkuu wa mauaji ya mwanafunzi huyo, pamoja na washirika wawili Brendan Muchiri na Kinaiya Kamau walifikishwa katika Mahakama ya Kiambu Jumatatu asubuhi.

Jaji aliwaruhusu polisi kuwazuilia washukiwa hao watatu kwa wiki mbili ili kuwapa nafasi ya kukamilisha uchunguzi.