Maisha ya giza ya jambazi aliyeuawa Samuel Mugoh Muvota

Muhtasari

• Matokeo yamefichua maisha ya giza ya mwanamume huyo tangu mwaka wa 2011, wakati Muvota alipoanza kuwaibia wahasiriwa kwenye mitambo ya ATM.

• Cha kushangaza ni kwamba hakuna hata mmoja kati ya wake hao aliyeshuku kuwa Muvota aliishi maisha ya sura mbili.

 

Kufuatia mauaji ya mwanamume mmoja huko Mirema Jumatatu alasiri, wapelelezi wa idara ya DCI wamekuwa wakichanganua hifadhidata ya uhalifu ya DCI ili kubaini Samuel Mugoh Muvota alikuwa nani. 

Maelezo yaliyotolewa na DCI ni ya kutamausha. Matokeo yamefichua maisha ya giza ya mwanamume huyo tangu mwaka wa 2011, wakati Muvota alipoanza kuwaibia wahasiriwa kwenye mitambo ya ATM katika benki mbalimbali na kuhitimu kuwa jambazi wa muda wote.  

Kulingana na uchunguzi wa DCI jamaa huyo aliajiri wanawake warembo na wenye sura za kupendeza. Aliwasambaza kama mawakala wa kuwawekea watu dawa za kulevya katika vinywaji katika sehemu mbalimbali za burudani za hadhi ya juu. 

Kufikia siku ya Jumatatu aliyomiminiwa risasi sita na mtu asiyejulikana, Muvota ambaye aliongoza sakata ya ulaghai kwa kubadilisha kadi za ATM na simu na kuendesha shughuli zake kama kundi la kihalifu la kimafia, alikuwa ni bilionea na mali nyingi. Alikuwa na majumba, magari kadhaa, wake 7 wote wakiishi maisha ya anasa kutokana na mapato ya wizi.

Cha kushangaza ni kwamba hakuna hata mmoja kati ya wake hao aliyeshuku kuwa Muvota aliishi maisha ya sura mbili.  

Biashara ya Muvota ilikuwa na faida kubwa kiasi kwamba aliingiza wanawake zaidi ya 50 warembo katika biashara yake ya 'Pishori', ambayo imesababisha ndoa kuvunjika, na kusababisha wanaume wengi kulazwa hospitalini na mwngine kuuawa kwa kunywa dawa ya kulevya ambayo inajulikana kwa jina la 'Tamuu'.  

Kulingana na DCI dawa hiyo hutolewa kwa wagonjwa wenye shida ya akili.   DCI inasema kwamba Jambazi huyo alishirikiana na maafisa kadhaa wa polisi na wakati wowote wapelelezi walipoanzisha msako wa kumsaka, angefahamishwa kwa wakati.  

Muvota alianza kazi yake hiyo yake mwaka wa 2011 kwa kuzunguka ATM za jiji na kutoa msaada kwa wateja ambao walikuwa na shida kutoa pesa kutoka kwa akaunti zao. Pia alishirikiana na maofisa wa benki wapotovu.