Moto wateketeza maabara katika shule ya upili ya Moi Girls

Muhtasari

•Matete alisema gharama ya uharibifu uliosababishwa na moto huo inakadiriwa kuwa zaidi ya Sh5 milioni.

Moto mkubwa
Moto mkubwa
Image: WIKIPEDIA

Maabara ya shule ya upili ya Moi Girls mjini Eldoret iliharibiwa baada ya kushika moto usiku wa kuamkia Ijumaa..

Chanzo cha moto huo kinashukiwa kuwa ni hitilafu ya umeme au uvujaji wa gesi.

Wazima moto kutoka kaunti ya Uasin Gishu walikimbia katika shule hiyo iliyo umbali wa chini ya kilomita tatu na kukabiliana na moto huo kwa zaidi ya saa tatu.

Mkuu wa polisi wa Ainabkoi Leonard Matete alisema bado wanachunguza kisa hicho.

Uongozi wa shule na polisi wamesema hakuna mwanafunzi au mfanyakazi yeyote aliyejeruhiwa katika tukio hilo.

“Kila mtu yuko salama lakini maabara imeharibiwa kabisa,” Matete alisema.

Kulikuwa na milipuko wakati moto huo ulizuka kwa sababu ya kemikali zilizohifadhiwa kwenye maabara.

Matete alisema gharama ya uharibifu uliosababishwa na moto huo inakadiriwa kuwa zaidi ya Sh5 milioni. Alisema moto huo ulianza majira ya saa tano usiku wa Alhamisi.

Maabara iliyoteketea iko kwenye ghorofa ya juu ya jengo ambalo lina afisi na maabara nyingine chini yake.