logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Makurutu 10 wa polisi watiwa mbaroni kwa kughushi vyeti vya KCSE

Vyeti hivyo vitatumika kama ushahidi dhidi yao mahakamani.

image
na Radio Jambo

Yanayojiri16 June 2022 - 13:41

Muhtasari


•Kumi hao ambao walikuwa wamejiandikisha kuwa makonstabo wa polisi walikamatwa Jumatano jioni na mafunzo yao kukatizwa mara moja.

•Vyeti hivyo ghushi vilichukuliwa na kuhifadhiwa kama ushahidi utakaotumika dhidi ya washukiwa mahakamani.

Makurutu wa polisi

Makurutu 10 wa polisi katika chuo cha mafunzo ya polisi cha Kiganjo wametiwa mbaroni kwa kughushi stakabadhi zao za elimu.

Kumi hao ambao walikuwa wamejiandikisha kuwa makonstabo wa polisi walikamatwa Jumatano jioni na mafunzo yao kukatizwa mara moja.

Kitengo cha DCI kimeripoti kuwa hatua hiyo ilichukuliwa baada ya Baraza la Kitaifa la Mitihani nchini Kenya (KNEC) kuthibitisha kuwa vyeti vya KCSE vya washukiwa sio halali.

"Uchunguzi wa vyeti vyao vya kughushi ulionyesha kuwa baadhi ya madaraja ya somo na wastani yalibadilishwa kimakusudi ili kuendana na mahitaji ya chini kabisa ya kujiunga na huduma ya polisi," Taarifa iliyotolewa na DCI Alhamisi ilisoma.

Vyeti hivyo ghushi vilichukuliwa na kuhifadhiwa kama ushahidi utakaotumika dhidi ya washukiwa mahakamani.

"Washukiwa hao wamepoteza nafasi zao katika huduma ya polisi baada ya kufeli mtihani wa uadilifu na miezi mitatu ya mafunzo makali nyuma ya ua nene wa Kayaba, ambao ni sifa ya chuo cha mafunzo cha polisi cha Kiganjo," Taarifa hiyo  ilisoma.

Kumi hao wametambulishwa kama Mochama Opiyo Clive, Muithi John Kitavi, Natembea M. Kelvin, Nyapola Felix Angatia, Mwaulid Galgalo Bide, Gobra Grindguest, Ndambuki Irene Nzisa, Felix Kipkoech Langat, Kabatha Paul Kimani na John Crispus Amisi.

Washukiwa ni miongoni mwa makurutu 5,000 ambao walijiunga na chuo cha Kiganjo mwezi Machi.

Haya yanajiri huku kukiwa na ongezeko la kesi za ughushi wa stakabadhi za elimu nchini hasa miongoni mwa wanasiasa wanaowania nyadhifa za kisiasa.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved