Mbunge Didmus Barasa kusalia rumande kwa siku 10 zaidi

Upande wa mashtaka ulituma maombi ya kuomba muda zaidi wa kuwaruhusu wapelelezi kukamilisha uchunguzi.

Muhtasari

•Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma imesema Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa atasalia rumande kwa siku 10 zaidi.

•Kesi hiyo itatajwa tena mnamo Agosti 24 kwa DPP kuthibitisha hali ya upelelezi kabla ya kutoa uamuzi wa kushtakiwa.

Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa katika kituo cha polisi cha Bungoma mnamo Agosti 12, 2022
Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa katika kituo cha polisi cha Bungoma mnamo Agosti 12, 2022
Image: TONY WAFULA

Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma imesema Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa atasalia rumande kwa siku 10 zaidi.

Hii ilikuwa baada ya upande wa mashtaka kutuma maombi ya kuomba muda zaidi wa kuwaruhusu wapelelezi kukamilisha uchunguzi na kuruhusu mashahidi zaidi wakiwemo maafisa wa NYS na IEBC kurekodi taarifa.

Mahakama iliamua kwamba wapelelezi pia walihitaji muda wa kukamilisha na kuwasilisha ripoti za uchunguzi na mwili na wa silaha iliyotumika katika mauaji.

Kesi hiyo itatajwa tena mnamo Agosti 24 kwa DPP kuthibitisha hali ya upelelezi kabla ya kutoa uamuzi wa kushtakiwa.

Jumatatu, Barasa alifikishwa katika Mahakama ya Bungoma kwa madai ya mauaji.

"Upande wa mashtaka ukiongozwa na Mkuu wa Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma Kanda ya Magharibi, Peter Kiprop, ulituma maombi kwamba mbunge huyo asalie rumande ili kuruhusu ODPP ishirikiane na Shirika la Ulinzi la Mashahidi (WPA) ili kulinda mashahidi walioonyesha hofu ya kutoa ushahidi," ODPP alisema.

Mshukiwa anawekwa kizuizini kabla ya uchunguzi kukamilika ili kuzuia aina yoyote ya kuingiliwa kwa mashahidi kama vile vitisho, madhara ya kimwili au hata kifo.

Barasa alikaa wikendi hii katika seli ya polisi mjini Kisumu kufuatia kukamatwa kwake siku ya Ijumaa.

Alikimbizwa Kisumu kwa kile polisi walichokitaja kuwa usalama wake.

Amekana madai kwamba alimpiga risasi na kumuua Brian Olunga katika kituo cha kupigia kura.