Savula asema yeye ni naibu gavana bali ni gavana mwenza wa Kakamega

Alidai kuwa kaunti hiyo imegawanywa katika maeneo mawili 50/50 kati yake na Gavana Fernandes Barasa.

Muhtasari

• Mbunge huyo  wa zamani siku chache zilizopita alidai kuwa alilazimika kujiunga na Azimio kinyume na matakwa yake.

Naibu Gavana wa Kakamega Ayub Savula
Naibu Gavana wa Kakamega Ayub Savula
Image: MAKTABA

Naibu gavana wa Kakamega Ayub Savula amedai kuwa yeye ni gavana mwenza.

Alidai kuwa kaunti hiyo imegawanywa katika maeneo  mawili 50/50 kati yake na Gavana Fernandes Barasa.

“Mtu asikudanganye kwamba Savula alirudi kuwa naibu, hapana. Tumegawanya serikali ya kaunti ya Kakamega kuwa mbili, Barasa amechukua nusu nami nimechukua nusu,” akasema.

Savula alisema nafasi za wizara katika kauni hiyo zitagawanywa kwa usawa kati yao.

Mbunge huyo  wa zamani siku chache zilizopita alidai kuwa alilazimika kujiunga na Azimio kinyume na matakwa yake.

Alisema alikuwa mshiriki wa Rais Mteule William Ruto baada ya kuchaguliwa tena kuwa Mbunge wa Lugari mwaka 2017 lakini muda mfupi baadaye, alikamatwa pamoja na wake zake wawili kama njia ya kumtisha.

“Nilikamatwa saa nane usiku katika hoteli moja. Usiku huohuo wake zangu wawili walikamatwa kutoka kwa nyumba zao, mmoja saa tisa asubuhi na mwingine saa kumi na moja asubuhi, kwa madai kwamba tuliiba Shilingi bilioni 1.5 kutoka kwa serikali. Ilibainika kuwa hakuna ushahidi wa kuunga mkono kesi hiyo,” Savula alisema.

“Pia ilidaiwa kuwa sikuwa nimelipa ushuru wa Shilingi 0.5 bilioni kwa Mamlaka ya Ushuru ya Kenya, na walifunga akaunti zangu zote ili kunibana. Nilipitia kuzimu.”

Alisema maafisa wakuu walimwambia kuwa atasamehewa iwapo ataacha kumuunga mkono Ruto na badala yake kumuunga mkono mgombeaji urais wa Azimio-One Kenya Raila Odinga.