Ruto kuanzisha huduma ya Hustler Fund Micro Credit

Ruto alisema Hustler Fund itafanyiwa utathmini kukagua historia ya ukopaji ya watumiaji milioni 18 kila baada ya miezi minne

Muhtasari

• Rais William Ruto alisema Hustler Fund itafanyiwa utathmini kukagua historia ya ukopaji ya watumiaji milioni 18 kila baada ya miezi minne na kuwatunuku madaraja ya kifedha.

RAIS WILLIAM RUTO

Jumla ya watu milioni sita wamejisajili kwa Hustler Fund na sasa wanaweza kupata pesa zaidi kufuatia ukaguzi wa historia yao ya kukopa. 

Rais William Ruto alisema Hustler Fund itafanyiwa utathmini kukagua historia ya ukopaji ya watumiaji milioni 18 kila baada ya miezi minne na kuwatunuku madaraja ya kifedha. 

Alieleza kuwa daraja la fedha ndilo litakaloamua ukomo wa mkopo wa mtu kulingana na jinsi anavyokopa mara kwa mara na kurejesha kwa wakati.

"Mwishoni mwa mwezi huu, kila mkopaji atapangiwa daraja la fedha. Hii itaeleza nini kinamfanya mtu apate alama nzuri," aliongeza. 

Rais pia alitangaza uzinduzi wa bidhaa mpya chini ya hazina ya hustler, Hustler Fund Micro Credit, ambayo itaruhusu mashirika ya akiba na mikopo (Sacco), na Vikundi kukopa kwa niaba ya wanachama wao. 

“Mwishoni mwa mwezi huu, Hustler Fund itakuwa na bidhaa ya pili itakayosaidia wale wa Saccos na vikundi pia kupata mikopo yenye riba nafuu na kuwasaidia wanachama wao kukuza biashara zao,” alisema. 

 

Rais Ruto alisema hayo wakati wa Sherehe za Kuadhimisha Miaka 50 Tangu Kuanzishwa kwa Sacco ya Polisi nchini Kenya na kufungua uwanja wa Police Sacco Stadium eneo la South C, Kaunti ya Nairobi. 

Rais alisema Serikali itaunga mkono vyama vya ushirika ili kuboresha upatikanaji wa mikopo na kukuza mazoea ya kuweka akiba miongoni mwa Wakenya.  

Rais Ruto alipongeza Police Sacco kwa kujenga Uwanja ambao utatumika kukuza talanta katika huduma ya polisi na eneo la South C. 

Alitoa wito kwa mashirika ya Akiba na Mikopo kuchangamkia teknolojia ili kuongeza ufanisi na kuboresha ufikiaji wa wanachama wake.