Raila aomboleza wanafunzi wa Chuo kikuu cha Pwani

Wahadhiri na wanafunzi ni miongoni mwa wahasiriwa.

Muhtasari

Watu kadhaa waliojeruhiwa walipelekwa katika hospitali za karibu kwa matibabu ya haraka.

Basi la Chuo Kikuu cha Pwani baada ya ajali.
Basi la Chuo Kikuu cha Pwani baada ya ajali.
Image: GEORGE MURAGE

Kiongozi wa Azimio Raila Odinga ametuma risala za rambi kwa chuo kikuu cha Pwani kufuatia ajali kwenye barabara kuu ya Nairobi-Nakuru siku ya Alhamisi.

Ajali hiyo iliyohusisha basi la shule na matatu aina ya Nissan eneo la Kayole-Karai huko Naivasha ilisababisha vifo vya takriban watu 14.

Wahadhiri na wanafunzi ni miongoni mwa wahasiriwa.

“Natuma rambirambi zangu za dhati kwa jamii ya Chuo Kikuu cha Pwani na wale wote waliopoteza marafiki, na wapendwa wao katika ajali ya kusikitisha iliyohusisha basi la Chuo Kikuu cha Pwani na matatu katika barabara kuu ya Naivasha-Nakuru,” Raila alisema kwenye ujumbe wake wa Twitter.

Ajali hiyo inasemekana kutokea baada ya kushukiwa kufeli kwa breki.

Mkuu wa polisi wa kanda ya Bonde la Ufa Tom Odera alisema huenda idadi ya waliofariki ikaongezeka.

"Basi lilibingiria na kuua 12 papo hapo. Huenda tukawa na majeruhi zaidi," alisema.

Odera alisema basi hilo lilikuwa na takriban watu 30 wakiwemo wahadhiri na wanafunzi waliokuwa wakielekea kwenye mashindano ya michezo.

Aliongeza kuwa dereva wa basi hilo alishindwa kulimudu na kugonga takriban magari matano kabla ya kubingiria kwenye mtaro.

Watu kadhaa waliojeruhiwa walipelekwa katika hospitali za karibu kwa matibabu ya haraka.

MHARIRI; DAVIS OJIAMBO.