Mwanamke amchoma kisu mtoto wake wa miaka 2 hadi kufa na kumjeruhi mwingine

“Tulienda kwenye nyumba hiyo na kukuta tayari ameua mtoto mmoja na mwingine yuko mahututi.

Muhtasari
  • Pia alijaribu kujitoa uhai kwa kujichoma kisu bila mafanikio lakini aliokolewa na majirani.
Mwanamke amchoma kisu mtoto wake wa miaka 2 hadi kufa na kumjeruhi mwingine
Image: MATHEWS NDANYI

Mwanamke mmoja  Eldoret amemdunga kisu na kumuua mwanawe wa miaka miwili kufuatia ugomvi wa nyumbani.

Mwanamke huyo aliyetambulika kama Cristabel Chebet pia alimjeruhi vibaya bintiye wa umri wa miaka sita wakati wa hasira kali dhidi ya watoto hao.

Pia alijaribu kujitoa uhai kwa kujichoma kisu bila mafanikio lakini aliokolewa na majirani.

Tukio hilo lilitokea katika eneo la generations estate mjini humo.

Mwanamke huyo alikuwa amerejea kutoka nyumbani kwake kijijini mapema leo na kugombana na mumewe kabla ya kuchukua kisu na kuwashambulia watoto.

Polisi walifika eneo la tukio na kuuchukua mwili wa marehemu hadi kwenye chumba cha kuhifadhi maiti huku mtoto aliyejeruhiwa akilazwa katika hospitali ya Rufaa ya Moi.

Chebet aliambia wanahabari katika eneo la tukio kwamba alikuwa amefadhaishwa na matatizo ya kifamilia na hakuwa na nia ya kuwaua watoto wake ingawa alizidiwa na hasira.

Aliomba msamaha kutoka kwa kila mtu na Mungu.

"Nimekuwa na matatizo lakini hakuna aliyetaka kunisikiliza. Nimefanya hivyo kutokana na hasira kali na kuomba msamaha," alisema.

Alimwomba Mungu awapumzishe watoto wake kwa amani.

Mwanamke huyo alisema mumewe alimpenda mtoto wake mdogo kuliko msichana ambaye alimlea kutoka kwa uhusiano wa awali.

Alisema baada ya kukasirika alichukua uamuzi wa kufa na watoto wake wote badala ya kuteseka bila msaada wowote.

Mwanachama wa Nyumba Kumi eneo hilo Grace Onyango alisema alisikia watu wakipaza sauti kuwa mama mmoja amewaua watoto wake.

“Tulienda kwenye nyumba hiyo na kukuta tayari ameua mtoto mmoja na mwingine yuko mahututi.

Onyango alisema mwanamke huyo alilalamika kuwa amechoka kuteseka maishani na bado hakuna aliyemsaidia.

OCPD wa kaunti ndogo ya Turbo Edward Masibo alithibitisha kisa hicho na kusema uchunguzi unaendelea.