Pigo kwa Mackenzie baada ya mawakili wawili kujiondoa kwenye kesi

Hata hivyo wakili wa tatu Wycliffe Makasembo amesema atashikamana na watuhumiwa hao hadi mwisho.

Muhtasari
  • Mawakili George Kariuki na Elisha Komora wametaja kufadhaika katika kujaribu kuwapata washukiwa hao.
katika mahakama ya Shanzu mnamo Juni 2, 2023
Mchungaji Paul MacKenzie katika mahakama ya Shanzu mnamo Juni 2, 2023
Image: SCREENSHOOT

Paul Mackenzie na washukiwa wengine kwenye kesi ambapo wanadaiwa kusababisha vifo vya mamia ya watu katika msitu wa Shakahola, Kaunti ya Kilifi, wamepata pigo Jumatano baada ya mawakili wao wawili na tegemeo, kujiondoa kwenye kesi hiyo.

Mawakili George Kariuki na Elisha Komora wametaja kufadhaika katika kujaribu kuwapata washukiwa hao.

Pia walisema wanakabiliwa na vitisho na wanahofia haki inaweza kutopatikana.

"Kwa changamoto ambazo washukiwa wanapitia na hali ya sasa, nahisi dhamiri yangu imevurugika," Kariuki alisema.

Alieleza hofu yake kuwa washukiwa hao wanaweza kufariki hata kabla ya kesi kusikizwa kutokana na hali duni ambayo wamekuwa wakikabiliana nayo.

"Wamekuwa wakilala sakafuni kwa siku 60. Inashinda haki... Hakika, wanaweza kuugua na kufa kabla ya kesi," alidai.

Hata hivyo wakili wa tatu Wycliffe Makasembo amesema atashikamana na watuhumiwa hao hadi mwisho.

"Nahisi kuna mkono usioonekana unajaribu kuwakatisha tamaa Mackenzie na wengine. Mkono huu si mwingine bali ni serikali. Binafsi nitashikamana na Mackenzie na wengine hadi kufa au nitakapohisi nimetosheka na pia kukimbia. " alisema.