Gavana Sakaja awaomba radhi wachuuzi wa Nairobi kutokana na dhulma za askari wake

Katika masaibu hayo, wafanyabiashara wengi walinyanyaswa, na kunyang’anywa bidhaa zao.

Muhtasari

•Haya yanajiri kufuatia tukio baya lililoshuhudiwa Oktoba 18, 2023, ambapo maafisa wa ukaguzi wa jiji walinaswa kwenye kamerawakizozana na wafanyabiashara na wachuuzi katika msako mkali dhidi ya wafanyabiashara wanaofanya biashara katika Wilaya ya Kati ya Biashara (CBD) bila hati halali kutoka kwa serikali ya kaunti. 

•“Nimeagiza kuachiliwa mara moja kwa vitu vyote vilivyotaifishwa, na kuwaomba radhi wafanyabiashara hao na kuwalipa binafsi fidia ya shilingi 10,000 kila mmoja,” 

Gavana Sakaja. Hisani:Instagram
Gavana Sakaja. Hisani:Instagram

Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja amewasuta maafisa wake wa ukaguzi kwa kuwahangaisha wachuuzi.

Msamaha wa Sakaja  unajiri baada ya tukio baya lililoshuhudiwa Oktoba 18, 2023, ambapo askari wa kaunti walinaswa kwenye kamera wakizozana na wafanyabiashara na wachuuzi katika msako mkali dhidi ya wafanyabiashara wanaofanya biashara katikati mwa jiji la Nairobi bila ya leseni za kaunti.

Katika masaibu hayo, wafanyabiashara wengi walinyanyaswa, na kunyang’anywa bidhaa zao.

Katika taarifa, hata hivyo, mkuu huyo wa kaunti, ambaye yuko katika safari rasmi ya Ufaransa, aliomba radhi kwa jinsi wachuuzi hao walivyoshughulikiwa na kutaka waachiliwe bila masharti.

Pia aliomba wafanyabiashara hao walipwe fidia.

“Nimeagiza kuachiliwa mara moja kwa vitu vyote vilivyotaifishwa, na kuwaomba radhi wafanyabiashara hao na kuwalipa binafsi fidia ya shilingi 10,000 kila mmoja,” alisema Sakaja.

Aliongeza kuwa hatua ya maafisa wake wa ukaguzi haikuwa muhimu na kwamba utawala wake umekuwa ukiwasihi maafisa kuwatendea wakazi wa Nairobi kwa utu.

"Tumekuwa na uhusiano mzuri na wafanyabiashara wasio rasmi kwa mwaka mmoja lakini hivi karibuni kumekuwa na matukio ya kusikitisha ambayo yanataka kuhujumu hilo.

Zaidi ya hayo, gavana aliahidi kuwachukulia hatua za kinidhamu maafisa waliokuwa wakisimamia operesheni hiyo.

"Hata kama wafanyabiashara walikuwa wakifanya kazi bila stakabadhi zinazohitajika, ikiwa ni pamoja na Cheti cha Matibabu kutoka kwa Afya ya Umma ambacho kila mhudumu wa chakula lazima awe nacho kwa usalama wa wakazi wa Nairobi, hawakustahili kuhudumiwa hivyo na tunashughulikia hili kwa undani."

Msamaha wa gavana Sakaja unajiri baada ya ukosoaji kutoka kwa wakenya kwenye mitandao ya kijamii ambao walilaumu afisi yake kwa kuwatendea wafanyabiashara wadogo jambo lisilo la utu.

Mbunge wa Dagoreti Mashariki Babu Owino,alimlaumu gavana kwa vitendo hivyo na kusema kwamba msamaha wake auna uzito wowote kwani tukio hilo lilichukua muda baada ya gavana kujitokeza na kuomba msamaha.

"Hizi PR ndogo ndogo wachana nazo.Kanjo hawezi kufanya kazi bila maagizo yako.Heshimu hustlers tunajua kuwa umekulia kwenye utajiri na huelewi kabisa  nini maana ya  kwenda bila chakula.Operesheni hii ilichukua siku nzima, mbona hujaisimamisha asubuhi hata baada ya kupewa taarifa?" Alisema

Hali hiyo ilitokea  hata baada ya gavana kutoa ahadi  kwa wachuuzi kuwa chini ya uongozi wake, wachuuzi hawatakamatwa kwa vile wanahangaika kulisha familia zao.