Wafungwa 13 walikosa kufanya mitihani ya KCPE, KPSEA

Kulingana na afisa anayesimamia gereza hilo Hassan Tari wafungwa hao wote walikuwa tayari kwa mitihani licha ya changamoto mbalimbali.

Muhtasari

• Wafungwa hao hawakuachiliwa au kuhamishiwa katika taasisi nyingine za adhabu, gereza hilo likiwa limesajili jumla ya watahiniwa 54 wa mitihani ya kitaifa.

• "Vifaa vya mitihani vilifika gerezani kwa wakati na wafungwa wote walikuwepo mbali na waliohamishwa au kuachiwa huru"

Wafungwa wa KCPE katika gereza la Naivasha wakipanga foleni kukaguliwa kabla ya kufanya mitihani yao
Wafungwa wa KCPE katika gereza la Naivasha wakipanga foleni kukaguliwa kabla ya kufanya mitihani yao

Jumla ya wafungwa 13 kutoka gereza la Naivasha  walikosa mitihani ya Cheti cha Elimu ya Msingi ya Kenya (KCPE) na Tathmini ya Elimu ya Shule ya Msingi ya Kenya (KPSEA) mnamo Jumatatu.

Wafungwa hao hawakuachiliwa au kuhamishiwa katika taasisi nyingine za adhabu, gereza hilo likiwa limesajili jumla ya watahiniwa 54 wa mitihani ya kitaifa.

Kati ya idadi hiyo, ishirini na moja wanatumikia kifungo cha maisha jela katika gereza hilo ambalo lina zaidi ya wafungwa 3,000 ambao wengi wao wako chini ya mpango wa elimu.

Kulingana na afisa anayesimamia gereza hilo Hassan Tari wafungwa hao wote walikuwa tayari kwa mitihani licha ya changamoto mbalimbali.

Alisema wafungwa 23 walikuwa wamesajiliwa kwa KCPE kupitia wawili waliokosa baada ya kuachiliwa huku 31 wakiwa wamesajiliwa kwa KPSEA ingawa 11 hawakuhudhuria.

"Vifaa vya mitihani vilifika gerezani kwa wakati na wafungwa wote walikuwepo mbali na waliohamishwa au kuachiwa huru" alisema.

Alisema kuwa idara ya magereza imetoa msaada wote unaohitajika kwa wafungwa hao kwani elimu imegeuka kuwa nyenzo ya kurekebisha tabia.

"Mitihani ilianza kwa wakati na wafungwa wameonyesha imani ya kufanya vyema huku ila kuna  changamoto chache zinazojitokeza," alisema.

Mmoja wa wafungwa hao, Gideon Langat ambaye anatumikia kifungo cha miaka 12 kwa wizi, aliwapongeza walimu ambao pia ni wafungwa kwa kazi waliyoifanya ya kuwaandaa wafungwa.

Alitoa changamoto kwa serikali katika siku zijazo kutenga fedha kwa idara ya elimu gerezani ambayo imekuwa chombo cha kurekebisha tabia.

"Pamoja na matatizo yote, tuko tayari kuwapa changamoto wanafunzi wenzetu ambao wana faida zaidi yetu, kwani shule zao zinafadhiliwa tofauti na sisi," alisema.

Afisa  wa elimu wa kaunti ndogo ya Naivasha Nancy Mutai alitaja zoezi hilo kuwa huru na la haki  akiongeza kuwa hakuna hitilafu yoyote iliyoripotiwa siku ya kwanza.

"Shule zote zilipokea vifaa vya mitihani kwa wakati ufaao na kufikia sasa hatunakili changamoto yoyote katika siku ya kwanza," alisema.