Watahiniwa wanne wa mtihani wa KCSE wakamatwa wakivuta bangi Kisumu

Wakati wa kukamatwa, vijiti saba vya bangi vilipatikana na kuwekwa kama ushaidi

Muhtasari

• Wiki iliyopita, Mkuu wa Utumishi wa Umma Felix Koskei alitangaza vita dhidi ya biashara haramu na matumizi ya dawa za kulevya

• Koskei alisema kuwa serikali itahakikisha kwamba uovu huo unakabiliwa. 

Image: The Star

Wanafunzi wanne wa kidato cha nne walikamatwa kwa madai ya kuvuta bangi shuleni  mjini Kisumu.

Wanafunzi hao wanne walikamatwa Jumatatu jioni na baadaye kuachiliwa na polisi ili kuruhusiwa kufanya  mtihani wa KCSE unaoendelea kabla ya kushtakiwa mahakamani ripoti ya polisi ilisoma.

Mwalimu Mkuu wa shule hiyo alisema kuwa wanafunzi hao walionaswa walikuwa wametumia funguo za shule  kufikia ofisi ya michezo ambapo walipatikana wakivuta bangi.

Wakati wa kukamatwa, misokoto saba ya bangi ilipatikana na kuwekwa kama ushahidi. Wanne hao ni wa umri wa kati ya  miaka 17 -18.

Kulingana na shirika la NACADA pombe, tumbako, bangi, miraa na dawa za kulevya ndizo zinazotumiwa vibaya zaidi shuleni.

Utafiti wa kitaifa wa miaka mitano kuhusu Hali ya Dawa na Matumizi ya Dawa za Kulevya nchini Kenya, 2022 uliotolewa hivi karibuni unaonyesha watoto 156,461 wa shule za msingi kwa sasa wanatumia  tumbaku.

127,124 wanatumia pombe,  Miraa 112,456 na 39,115 wanavuta bangi.

Mtafiti Mkuu wa Nacada Morris Kamenderi alisema kwa jumla, vijana 153,846 wenye umri wa miaka 15 hadi 24 tayari wameathirika sana na pombe.

Huku vijana 90,531 wakitajwa kuathirika na uvutaji wa bangi.

Wiki iliyopita, shirika la afya duniani lilipendekeza kupiga marufuku uuzaji wa bidhaa hizo karibu na shule.

Sheria ya Kudhibiti Tumbaku nchini Kenya tayari imepiga marufuku uuzaji wa bidhaa za tumbaku karibu na shule.