Mwanamke aanguka na kufariki akiwa nyumbani kwake Nairobi

Alianguka kwenye sebule yake wakati mumewe alikuwa na shughuli nyingi kwenye chumba cha kusomea

Muhtasari

•Mwanamke huyo alikuwa ndani ya nyumba katika ghorofa ya Ndonyo Park na mumewe wakati kisa hicho kilitokea Jumapili usiku.

•Alilalamikia uchungu uliomsukuma mwanamume huyo kumpatia huduma ya kwanza huku akiita gari la wagonjwa kumpeleka hospitalini

crime scene
crime scene
Image: HISANI

Polisi wanachunguza kisa ambapo mwanamke raia wa Japani alianguka na kufa ndani ya nyumba yake katika eneo la Spring Valley, Nairobi.

Mwanamke huyo alikuwa ndani ya nyumba katika ghorofa ya Ndonyo Park na mumewe wakati kisa hicho kilitokea Jumapili usiku.

Yoshimo Saito inasemekana alianguka kwenye sebule yake wakati mumewe alikuwa na shughuli nyingi kwenye chumba cha kusomea. Mume wa marehemu aliwaambia polisi kwamba alimsikia akipiga kelele na alipokimbia kuangalia kinachoendelea, alimkuta akiwa ameshika kifua.

 Alilalamikia uchungu uliomsukuma mwanamume huyo kumpatia huduma ya kwanza huku akiita gari la wagonjwa kumpeleka hospitalini. Ambulensi ilifika na madaktari walithibitisha kuwa alikuwa amekufa.

Polisi waliitwa kwenye eneo la tukio na kulishughulikia kabla ya mwili kuhamishwa hadi kwenye chumba cha kuhifadhia maiti kusubiri uchunguzi na majibu.

Kwingineko katika mtaa wa Tena, Nairobi, mwili wa Dennis Wabwire mwenye umri wa miaka 48 ulipatikana chumbani mwake muda mrefu baada ya kufariki.

 Polisi waliitwa eneo la tukio kusaidiwa kuusafisha na kuupeleka mwili wa marehemu kwenye chumba cha kuhifadhia maiti. Sababu ya kifo hicho bado hakijajulikana, polisi walisema.

Huko Makuyu, kaunti ya Muranga, dereva wa trekta alipatikana akiwa amekufa nyumbani kwake baada ya kulalamikia maumivu ya kifua.

Mwanamume huyo aliyetambulika kama Benson Gicheru alikuwa amefika nyumbani na kumwarifu mkewe alikuwa na maumivu ya kifua. Baadaye alistaafu kulala na kumwomba mkewe kumwamsha saa 4 asubuhi ili aende kazini katika shamba la jirani.

Mke aliwaambia polisi kwamba alijaribu kumwamsha bila mafanikio. Alikuwa amekufa usiku. Polisi walisema wanachunguza tukio hilo na bado hawajabaini chanzo cha kifo hicho. Mwili huo ulihamishwa hadi kwenye chumba cha kuhifadhia maiti ukisubiri uchunguzi wa maiti na taratibu nyinginezo.