Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja amesema mmoja wa watu walioonekana wakiteketeza City Hall anafanya kazi katika ofisi ya Mbunge.
Akihutubia wanahabari siku ya Alhamisi, Sakaja alitaka mbunge huyo na msaidizi wake wajulikane ili sheria ichukue mkondo wake.
“Mwanasiasa na mbunge aliyewatuma wajulikane,” alisema.
Wakati huo huo alikanusha madai kwamba alifanikisha wahuni waliojipenyeza na kujiunga na maandamano ya Gen Z siku ya Jumanne.
Gavana huyo alisema alikuwa Pwani na baraza lake la mawaziri na hangeweza kupata muda kupanga jambo kama hilo.
Anaongeza kuwa anaamini katika Siasa safi na hivyo hawezi kuwa mshiriki wa mambo kama hayo.
Alionekana kuwalaumu wapinzani wake wa kisiasa kwa kueneza madai hayo.
Alisema kuwa amepokea ombi la kuomba Uhuru Park kwa Genz kuwaheshimu wenzao waliofariki, ombi ambalo alisema atalikubali.
Sakaja alisema atahudhuria hafla hiyo itakapofanyika.