'Huwezi kuwa Serikalini na kuwa Upinzani,' Salasya aambia ODM

Wachache ni upinzani ambao unaweka serikali katika udhibiti, na jinsi ilivyo, ODM hailingani na msimamo huo.

Muhtasari
  • Mbunge huyo wa Mumias Mashariki alieleza kufeli kwa Muungano wa Azimio la Umoja huku upinzani ukihoji ukimya wa Kalonzo Musyoka.
MBUNGE PETER SALASYA
Image: HISANI

Mbunge wa Mumias Mashariki Peter Salasya sasa amekitaka chama cha ODM kuamua ikiwa wanataka kuwa Serikalini au kusalia upinzani.

Katika video, Salasya anasema hakuna njia yoyote ODM ingetaka kuwa serikalini na wakati huo huo kuisimamia.

“ODM lazima iamue, hakuna jinsi moyo wako unaweza kuwa upande huu na upande mwingine kwa wakati mmoja. ODM kutaka kua kama fisi. Yani ako kwa serikali ako kwa upinzani,” Peter Salasya alisema.

Mbunge huyo anaeleza zaidi kuwa bunge linaundwa na wawakilishi wa wengi na walio wachache.

Wachache ni upinzani ambao unaweka serikali katika udhibiti, na jinsi ilivyo, ODM hailingani na msimamo huo.

“Huwezi kuwa serikalini na kuwa upinzani, isipokuwa tubadilishe katiba na kusema bunge halina watu wachache. Ninataka kuwaambia wanachama wa ODM, mnafaa kuchagua kama mtanisaidia kusimamia serikali au kujiunga na serikali,” akasema.

Mbunge huyo wa Mumias Mashariki alieleza kufeli kwa Muungano wa Azimio la Umoja huku upinzani ukihoji ukimya wa Kalonzo Musyoka.

Anasema kufikia sasa Kiongozi wa Wiper alifaa kuzungumzia njia ya Muungano kwani ODM imehamia kula na serikali.

"Hakuna kitu kama Azimio leo, kwa sababu sijaona Kalonzo akitoa taarifa yake hakuna ndoa hapa."

Zaidi ya hayo, Salasya anamwomba Gen Z wamteue kuwawakilisha bungeni kuwa kiongozi wa vijana ambao anaamini ni upinzani kwa sasa.

"Gen Z wanapaswa  kuniteua kama mwakilishi wao katika bunge, ili niwe upinzani katika kuongoza masuala ya wananchi wa kawaida," alipendekeza.

Hata hivyo, Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna amekanusha madai kuwa ODM imejiunga na serikali.