Viongozi wa kike wa Homabay warai ODM kumteua Wanga kama naibu wa chama

Ombi hili linajiri baada ya kuondoka kwa manaibu viongozi wa zamani wa chama, Hassan Joho na Wycliffe Oparanya

Muhtasari

•Ombi hili linajiri baada ya kuondoka kwa manaibu viongozi wa zamani wa chama, Hassan Joho na Wycliffe Oparanya

•Ogutu alisema kuwa Wanga amethibitisha sifa za uongozi zinazohitajika wakati wa utawala wake kama mwenyekiti wa ODM katika Kaunti ya Homa Bay.

Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga
Image: FACEBOOK// GLADYS WANGA

Viongozi wanawake katika Kaunti ya Homa Bay wanataka uongozi wa chama cha Orange Democratic Movement (ODM) kumteua Gavana Gladys Wanga kuwa naibu kiongozi wa chama ili kusaidia kufanikisha sheria ya jinsia ya theluthi mbili.

Ombi hili linajiri baada ya kuondoka kwa manaibu viongozi wa zamani wa chama, Hassan Joho na Wycliffe Oparanya, ambao wanangoja kuchukua nyadhifa serikalini kama mawaziri.

Wanawake hao wameeleza kwa uongozi wa chama kuunga mkono uteuzi wa Wanga bila kujali njia watakayotumia katika kujaza nafasi zilizokuwa za Oparanya na Joho.

Viongozi hao wa wanawake wakiongozwa na Mwenyekiti wa ODM Women League katika Kaunti ya Homa Bay, Peres Ogutu, Mwenyekiti wa Rangwe Constituency Caroline Owidhi, na wabunge wa ODM wakiongozwa na Joan Ogada, wameomba kiongozi wa ODM, Raila Odinga, kuangazia uteuzi wa Wanga kwa wadhifa huo.

Wakizungumza na waandishi wa habari mjini Homa Bay, Ogutu alisema kuwa Wanga amethibitisha sifa za uongozi zinazohitajika wakati wa utawala wake kama mwenyekiti wa ODM katika Kaunti ya Homa Bay.

Aliongeza kuwa hilo limewafanya kuwa na imani kwamba Wanga ataweza kutekeleza majukumu ya kuwa naibu kiongozi wa ODM kwa ufanisi.

Ogada alisisitiza kuwa kupandishwa kwa Wanga kwa wadhifa huo kutasaidia wanawake kufanikisha sheria ya jinsia ya theluthi mbili, sio tu katika chama cha ODM bali pia katika nafasi nyingine za kuchaguliwa nchini Kenya.