Mwanamume amuua jirani yake kwa madai ya kuiba makaa, Machakos

Marehemu alikuwa na majeraha makubwa kichwani na alivunjika mguu wa kushoto huku akiwa na damu usoni.

Muhtasari

•Jerobon alisema mwanamume huyo mwenye umri wa miaka 35 aliripoti kisa hicho kwa kituo cha polisi cha Kathama baada ya kufanya uhalifu huo mbaya.

•Maafisa walitembelea eneo la tukio na kukuta Kithande alikuwa amepelekwa nyumbani kwake na alifariki dunia kutokana na majeraha hayo.

Crime scene
Crime scene
Image: HISANI

Polisi katika eneo la Mwala, Kaunti ya Machakos wanachunguza kisa ambapo mwanamume mmoja alimvamia jirani yake kwa madai ya kuiba makaa yake siku ya Jumapili.

Kamanda wa polisi wa kaunti ndogo ya Mwala, Nancy Jerobon alisema mwanamume huyo mwenye umri wa miaka 35 aliripoti kisa hicho kwa kituo cha polisi cha Kathama baada ya kufanya uhalifu huo mbaya.

"Ilifanyika mnamo Agosti 11, 2024, katika kijiji cha Kithuiani katika kitongoji cha Ulaani, mtu mzima Mathias Mwanzia Kitheka mwenye umri wa miaka 35 alidai kuwa makaa yake yalikuwa yameibwa na akagundua kuwa jirani yake Attanus Mutiso Kithande mwenye umri wa miaka 51 ndiye aliiba,” Jerobon alisema kwa njia ya simu saa chache baada ya tukio hilo.

Jerobon alisema baadaye mshukiwa alimfuata marehemu na kumkatakata. Alikufa papo hapo.

"Alimfuata na kumvamia kwa kumkata kichwani na mguu wa kushoto kwa kutumia panga akimuacha akiwa amelala chini. Kisha mshukiwa akaenda kuripoti katika kituo cha polisi cha Kathama ambako aliwekwa chini ya ulinzi," Jerobon alisema.

Alisema maafisa kutoka kituo cha polisi cha Kathama walitembelea eneo la tukio na kukuta kwamba Kithande alikuwa amepelekwa nyumbani kwake na alifariki dunia kutokana na majeraha hayo.

"Alikuwa na majeraha makubwa kichwani na alivunjika mguu wa kushoto huku akiwa na damu usoni. Kiatu cha kushoto kilichokuwa na damu kilipatikana kutoka kwa nyumba ya mshukiwa," bosi huyo wa polisi aliongeza.

Mwili wa marehemu ulihamishwa hadi katika chumba cha kuhifadhi maiti cha hospitali ya Matuu Level 4 katika kaunti ndogo ya Yatta ukisubiri kufanyiwa uchunguzi.

Jerobon alisema mshukiwa atafikishwa mahakamani siku ya Jumatatu.

Alisema Idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai katika kituo cha polisi cha Mwala ilianzisha uchunguzi kuhusu tukio hilo.