Tume ya Kupambana na Ufisadi yamwagiza mbunge Didmus Barasa kufika mbele yake

EACC ilieleza kuwa inachunguza tuhuma za hongo zilizotolewa dhidi yake.

Muhtasari

•EACC ilisema kuwa Barasa anafaa kufika mbele yao siku ya Jumanne kwa ajili ya kurekodi taarifa.

•Kulingana na shirika hilo, hii ni nafasi ya pili kupewa mbunge huyo.

Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa
Image: MAKTABA

Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) imemuita mbunge wa Kimilili Didmus Barasa.

EACC ilisema kuwa Barasa anafaa kufika mbele yao siku ya Jumanne kwa ajili ya kurekodi taarifa.

Tume ilieleza kuwa inachunguza tuhuma za hongo zilizotolewa dhidi yake.

Kulingana na shirika hilo, hii ni nafasi ya pili kupewa mbunge huyo.

"Tume inakupa fursa ya pili kuja kujibu madai ya hongo iliyotolewa dhidi yako. Ili kufikia hili, unatakiwa kufika katika afisi za Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi katika Integrity Centre, Nairobi mnamo tarehe 27 Agosti 2024 saa tatu asubuhi," barua ya EACC iliyofikia Radio Jambo ilisomeka.

Barua ni ya tarehe 21 Agosti 2024.

Pia imemuonya dhidi ya kushindwa kuheshimu wito huo.

"Tafadhali kumbuka kuwa, ikiwa hautajitokeza kujibu tuhuma hizi, uchunguzi huu utaendelea hadi mwisho wake, na mapendekezo sahihi yaliyotolewa bila kujibu kwako," inasema.

"Maafisa wetu Celestine Owiti na Moses Tile watapatikana kukupokea na kurekodi taarifa yako."