Matokeo ya watahiniwa 840 wa KCSE 2024 yamefutiliwa mbali.
Waziri wa elimu Julius Ogamba mnamo Alhamisi alisema kuwa watahiniwa ambao matokeo yao yamefutiliwa mbali walihusika katika makosa ya mitihani.
"Kulikuwa na watahiniwa 840 ambao walihusika katika makosa ya mtihani 2024 na matokeo yao yamefutiliwa mbali," Ogamba alisema.
Waziri huyo alizungumza siku ya Alhamisi wakati wa kutolewa kwa matokeo ya KCSE 2024 katika Mtihani House jijini Nairobi.
Ogamba alifichua kuwa matokeo ya watahiniwa wengine 2829 wanaoshukiwa kuhusika na makosa ya mitihani yameshikiliwa.
“Baraza limepewa mamlaka kisheria kama ilivyoelezwa katika sheria za Baraza la Kitaifa la Mitihani la Kenya za 2015, notisi ya kisheria nambari 132 ya 2015, kanuni namba 8, kushikilia matokeo ya watahiniwa wa vituo vya mitihani wanaoshukiwa kuhusika na makosa ya mtihani ama ukiukwaji wa taratibu za mitihani huku uchunguzi ukisubiri kukamilika,” alisema.
"Kuhusu hili, matokeo ya watu 2829 wanaoshukiwa kuhusika na makosa ya mitihani yameshikiliwa hadi kukamilika kwa uchunguzi ambao utakamilika ndani ya muda wa siku 30 tangu kutolewa rasmi kwa matokeo ya mtihani ambayo ni leo," aliongeza.
Ogamba pia alisema kuwa wataalam wa elimu 91 walio chini ya kandarasi (walimu) wanaripotiwa kuhusika katika kusaidia makosa ya mitihani.
"Hatua kali za kinidhamu zitachukuliwa dhidi ya walimu kama hao," Ogamba alisema.