DCI wajibu kwa vitisho baada ya kukejeliwa kwa madai ya kumkamata ‘Mathe wa Ngara’

Wapelelezi wa DCI waliMthubutu mtumiaji huyo wa mitandao kujitokeza 'Kwa Mathe' bila silaha.

Muhtasari

•Bi Teresia Wanjiru na vijana watatu wadogo wenye umri wa kati ya miaka 16 na 17 waliwekwa rumande kwa mahojiano zaidi.

•DCI walikejeliwa kuwa licha ya kudaiwa kumkamata ‘Mathe’, hawawezi kulifunga eneo maarufu linalojulikana kama ‘Kwa Mathe.’

ambaye alikamatwa na wapelelezi Jumanne.
BI Teresia Wanjiru ambaye alikamatwa na wapelelezi Jumanne.
Image: TWITTER// DCI

Siku ya Jumanne, Kurugenzi ya Upelelezi wa Jinai iliripoti kukamatwa kwa washukiwa wanne baada ya shehena kubwa ya bangi na shilingi milioni 13.4 pesa taslimu kupatikana katika mitaa ya mabanda ya Kariua, mtaa wa Ngara, jijini Nairobi.

Bi Teresia Wanjiru na vijana watatu wadogo wenye umri wa kati ya miaka 16 na 17 waliwekwa rumande kwa mahojiano zaidi kufuatia operesheni hiyo na wanatarajiwa kufikishwa mahakamani siky ya Jumatano.

Washukiwa hao wanne walikamatwa katika eneo la uhalifu wakati wa operesheni ambayo iliendeshwa na wapelelezi kutoka Kitengo cha Kupambana na Dawa za Kulevya na Kitengo cha Kitengo cha Uhalifu Uliopangwa wa Kimataifa kwa usaidizi wa Kitengo cha Polisi cha Kupambana na Ugaidi kutoka Parklands ambao walivamia eneo hilo kufuatia taarifa za kijasusi.

Baadhi ya vitu zilizopatikana katika operesheni hiyo ya Jumanne ni pamoja na mifuko miwili iliyokuwa na mamilioni ya pesa zilizofichwa ndani yake, mifuko 26 ya bangi, katoni 4 za karatasi za kusokota, peremende 173 zilizopakiwa na katoni ya vitafunio vinavyoshukiwa kuwa ‘weed cookies.’

Kufuatia kukamatwa kwa wanne hao, mitandao ya kijamii ilishika moto huku wanamitandao Wakenya wakidai kuwa mwanamke aliyekamatwa, Bi Teresia Wanjiru ni muuza madawa ya kulevya maarufu, ‘Mathe wa Ngara.

Kulikuwa na hisia mseto kutoka kwa wanamtandao wa Kenya huku baadhi yao wakitaka kujua kama kweli mshukiwa huyo ndiye mlanguzi huyo maarufu wa dawa za kulevya wakati wengine wakiwadhihaki walinda sheria kuhusu kukamatwa kwake. Baadhi ya watu walimlinganisha mshukiwa aliyekamatwa na mfanyabiashara maarufu wa dawa za kulevya kutoka Mexico ‘El Chapo.’

Mtumizi wa twitter aliwajibu DCI akiwafahamisha kuwa licha ya kudaiwa kumkamata ‘Mathe’, hawawezi kulifunga eneo maarufu linalojulikana kama ‘Kwa Mathe.’

"Unaweza kumkamata mathe lakini huwezi kumkamata kwa mathe," @iamgrande aliandika.

Katika jibu lao, wapelelezi hao walithubutu mtumiaji huyo wa Twitter kujitokeza katika eneo hilo maarufu bila silaha.

“Sawa. Tupatane kwa mathe. Na mtu asije na mawe,” DCI alijibu.

Licha ya uvumi unaoenea kwemye mitandao ya kijamii, hakuna uthibitisho wa wazi uliotolewa na mamlaka kwamba mshukiwa aliyekamatwa anahusishwa kwa vyovyote vile na ‘Mathe wa Ngara’ maarufu.