logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Fahamu kwa nini serikali imesitisha usajili wa World Coin nchini Kenya

Waziri Kindiki ametangaza kuwa serikali imesitisha mara moja shughuli zote za World Coin.

image
na Radio Jambo

Yanayojiri02 August 2023 - 06:50

Muhtasari


•Kindiki aliibua wasiwasi wa serikali kuhusu shughuli hiyo yenye utata ambayo imeshuhudia maelfu ya Wakenya wakijitokeza kujisajili.

"Hatua ifaayo itachukuliwa kwa mtu yeyote ambaye anaendeleza, kusaidia, au vinginevyo kujihusisha au kuhusishwa na shughuli za World Coin," Kindiki alisema.

wengi walijitokeza kujisali na World Coin katika KICC siku ya Jumanne, Agosti 1, 2023.

Serikali ya Kenya, kupitia wizara ya Mambo ya Ndani na Utawala wa Kitaifa imesitisha rasmi zoezi la usajili la Sarafu ya Dunia (World Coin) ambalo limekuwa likiendelea katika siku chache zilizopita.

Katika taarifa yake siku ya Jumatano asubuhi, Waziri wa Mambo ya Ndani Kindiki Kithure aliibua wasiwasi wa serikali kuhusu shughuli hiyo yenye utata ambayo imeshuhudia maelfu ya Wakenya wakijitokeza katika maeneo mbalimbali ya usajili wa sarafu hiyo ya kidijitali nchini

Alisema uchunguzi wa uhalali na uhalisi wa mchakato huo umeanza huku shughuli zote zinazohusiana na sarafu hiyo tata zikisitishwa kwa wakati usiobainishwa

"Vyombo husika vya usalama, huduma za kifedha na ulinzi wa data vimeanza uchunguzi ili kubaini ukweli na uhalali wa shughuli hiyo, usalama na ulinzi wa data inayovunwa, na jinsi wavunaji wanavyokusudia kutumia data," Kindiki alisema katika taarifa.

Aliongeza, "Zaidi ya hayo, itakuwa muhimu kwamba uhakikisho wa usalama wa umma na usawa wa shughuli za kifedha zinazohusisha idadi kubwa ya raia utolewe kwa njia ya kuridhisha mapema."

Waziri alisema kuwa serikali imesitisha mara moja shughuli zote za World Coin na mashirika mengine yanayohusika na shughuli kama hiyo nchini Kenya hadi mashirika husika ya umma yatakapothibitisha kutokuwepo kwa hatari zozote kwa umma kwa ujumla.

"Hatua ifaayo itachukuliwa kwa mtu yeyote ambaye anaendeleza, kusaidia, au vinginevyo kujihusisha au kuhusishwa na shughuli zilizoelezwa hapo juu," ilisomeka taarifa hiyo.

Katika siku chache zilizopita, maelfu ya Wakenya wamefika katika vituo mbalimbali vya usajili vya World Coin nchini kote wakitumai kuchuma pesa zilizotajwa kutokana na usajili wa sarafu hiyo ya kidijitali.

Baadhi ya Wakenya waliohojiwa na Radio Jambo wamekiri kupata pesa, wengi wao kati ya shilingi 5000 na shilingi 7000 huku wengine bado wakiwa wameshikilia sarafu za kidijitali walizopewa baada ya kujisajili.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved