logo

NOW ON AIR

Listen in Live

"Sijui kwa nini niko hapa, Yesu atanisaida" MacKenzie azungumza baada ya kufikishwa mahakamani

MacKenzie aliweka wazi kwamba hafahamu  chochote kinachoendelea katika shamba lake la Shakahola.

image
na Radio Jambo

Habari02 June 2023 - 11:00

Muhtasari


•Akiwa mahakamani, MacKenzie alizungumza na wanahabari ambapo alieleza kutoridhishwa kwake na jinsi kesi hiyo inavyoendelea.

•MacKenzie alibainisha kuwa anaamini Mungu wake atampigania na hatimaye ataibuka mshindi katika kesi inayomkabili.

katika mahakama ya Shanzu mnamo Juni 2, 2023

Mchungaji wa Malindi mwenye utata Paul MacKenzie aliwasilishwa mbele ya Mahakama ya Shanzu siku ya Ijumaa ambapo upande wa mashtaka uliwasilisha ombi aendelee kuzuiliwa kwa siku 60 zaidi.

Akiwa mahakamani, MacKenzie alizungumza na wanahabari ambapo alieleza kutoridhishwa kwake na jinsi kesi hiyo inavyoendelea.

"Kwa kweli ata sioni maendeleo. Ata sijui kwa nini niko hapa mwanzo. Wacha tusubiri tuone," MacKenzie alisema.

Mwanzilishi huyo wa kanisa la Good News International alilalamika kuwa mambo yanavyokwenda anahisi kudhulumika.

"Sijaona lolote limeniweka hapa. Nasubiri nisikie," alisema.

Hata hivyo, alibainisha kuwa anaamini Mungu wake atampigania na hatimaye ataibuka mshindi katika kesi inayomkabili.

"Najua Yesu wangu ninayemtumikia na ninayemuamini atanisaidia," alisema.

MacKenzie aliweka wazi kwamba hana ufahamu wa chochote kinachoendelea katika shamba la Shakahola ambako baadhi ya wafuasi wake wanadaiwa kuzikwa.

Alibainisha kuwa amekuwa chini ya ulinzi wa polisi kwa miezi mawili hivyo hajapata nafasi ya kufuatilia yanayoendelea.

Alipoulizwa anayopitia rumande alisema, "Kwa kweli singetaka nizungumzie hayo kwa vyombo vya habari. Nafikiri kidogo yanahitaji muda wake."

Katika ombi la kutaka kuongezewa muda, upande wa mashtaka unasema  bado haujahitimisha uchunguzi na wanahitaji muda zaidi.

"Kurudishwa rumande kwa muda wa siku 60 ni muda mdogo zaidi unaowezekana ambao upelelezi unaweza kukamilika chini ya mazingira yaliyopo na ni njia ndogo zaidi za kudumisha Uadilifu wa upelelezi dhaifu," zilisomeka karatasi za mahakama.

Waendesha mashtaka wanadai kuwa hakuna mabadiliko ya hali ya kuachiliwa huru kwa Mackenzie pamoja na washukiwa wengine 17 tangu uamuzi wa mahakama hiyo mnamo  Mei 10 wakati waliporudishwa rumande.

"Bado kuna sababu za msingi za kuwanyima dhamana hadi upelelezi ukamilike na kuna uwezekano mkubwa wa mashtaka makubwa dhidi ya washukiwa," zinasomeka karatasi  za mahakama.

Kufikia sasa miili ya watu zaidi ya 243 imeshafanyiwa upasuaji katika mochari ya Hospitali Kuu ya Malindi katika Kaunti ya Kilifi.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved