Ukarimu wa Sonko! Ajitokeza na kumsaidia kocha wa zamani wa Harambee Stars

Gavana wa Nairobi Mike Sonko amejitokeza kumsaidia aliyekuwa kocha wa zamani wa Harambee Stars Marshall Mulwa.

Licha ya kuiletea Kenya sifa sufufu katika rubaa za kimataifa kupitia unahodha wake katika timu hiyo ya kitaifa, Mulwa alikuwa akiishi maisha ya kusikitisha.

Kocha huyo wa zamani ambaye ana umri wa miaka 75 alibaki upweke baada ya familia yake kuamua kuishi ughaibuni.

Kutokana na umri wake, Mulwa hakuwa na njia nyingine ila kuwategemea wahisani ili kupata lishe na kusukuma gurudumu la maisha.

Wakati kikosi cha Sonko kilimtembelea katika nyumba yake ya kukodisha, Mulwa alipokea chakula huku Sonko akiahidi kusaka njia zingine mwafaka zitakazomfaa ili kuboresha maisha yake.

"Mpira wa miguu unachukua jukumu muhimu katika jamii yetu kwa kuunganisha nchi yetu na pia kwa kuwapa vijana fursa ya kupata riziki," Sonko alibaini katika chapisho la Facebook.

"Kandanda imekuwa na umuhimu mkubwa mno katika kuleta umoja nchini mwetu na vile vile kuwapa ajira vijana," Sonko alisema kwenye ukurasa wake wa Facebook.

"Tutazungumza naye ili kujua ni vipi tunaweza kumsaidia ili aboreshe maisha yake," aliongeza.

Wakati akiwa nahodha wa kikosi cha Stars, timu hiyo ilipata ushindi mara tatu katika Cecafa Senior Challenge kati ya mwaka wa 1981 hadi 1983.