Manchester United itapambana na AC Milan katika awamu ya 16 bora ya ligi ya Uropa, huku Arsenali ikikabana koo na Olympiakos nao Tottenham wakimaliza udhia dhidi ya Dinamo Zagreb.
Kulingana na droo iliyotolewa jana, Rangers itapambana na Slavia Prague, Ajax ikialika Young Boys nao Dynamo Kiev wakipambana na Villarreal. Roma itapiga na Shakhtar Donetsk huku Granada ikialika Molde.
Mkondo wa kwanza utachezwa Machi tarehe 11 kabla ya mkondo wa pili kukamilika Machi 18.
Ufuatao ni msururu wa havari za spoti ulimwenguni.
Kwingineko, bwenyenye wa Chelsea Roman Abramovich amewapa wasmamizi wa klabu hio idhini ya kuwania sahihi ya mshambulizi matata wa Norway Erling Haaland msimu huu wa joto.
Nyota huyo wa Borussia Dortmund mwenye umri wa miaka 20 amefanya vyema katika klabu hiyo tangu kujiunga nao kutoka RB Salzburg mwezi Januari mwaka jana na inaaminika Abramovich yuko tayari kutoa zaidi ya pauni million 100 ili kumsajili.
Nahodha wa Liverpool Jordan Henderson amefanyiwa upasuaji kutokana na jeraha alopata wakati walipoteza 2-0 dhidi ya Everton wikendi iliyopita ugani Anfield.
Kiungo huyo wa Uingereza mwenye umri wa miaka 30 sasa atasalia nje kwa muda wa angalau mwezi mmoja na atarajea uwanjani mwezi Aprili. Kulingana na madaktari wa klabu hiyo Henderson atakosa mechi dhidi ya Sheffield United, Chelsea, Fulham na Wolves
Mbio za kwanza za msimu huu za Track and Field zitafanyika ugani Nyayo kesho asubuhi huku wanariadha kutoka kote nchini wakijumuika. Hapo awali mbio hizo zilistahili kufanyika katika chuo kikuu cha Bondo katika kaunti ya Siaya, lakini AK iliamua kuzirejesha Nairobi kutokana na kanuni kali za covid-19 na ukosefu wa nafasi ya kutosha.