Failure ni yule asiyejaribu, mimi nilijaribu ila haikuwa siku yangu – Kipchoge kuhusu Paris Olympics

"Mtu amefeli ni yule ambaye hajajaribu. Mimi nilijaribu kushinda olimpiki ya 3 lakini haikuwa siku yangu, na hiyo ndio hali ya spoti,” alisema.

wakati wa marathoni ya Olimpiki ya Paris
Eliud Kipchoge wakati wa marathoni ya Olimpiki ya Paris
Image: HISANI

Mwanariadha wa masafa marefu Eliud Kipchoge amevunja kimya chake baada ya kurejea nchini kutoka Ufaransa alikokuwa mmoja wa timu Kenya kushiriki mashindano ya Olimpiki Makala ya 2024.

Akizungumza na waandishi wa habari katika uwanja wa ndege wa JKIA, Kipchoge alisema kwamba kwa wale hawajui spoti vizuri, wanadhani Olimpiki ni kuhusu kushinda medali, jambo ambalo alipinga.

Mwanariadha huyo mkongwe alisisitiza kwamba ubora wa michezo ya Olimpiki si tu kushinda medali bali pia kuwepo na kushiriki ni fahari kubwa.

“Acha niwaambie kitu kimoja, Olimpiki sio kuhusu kushinda medali, ni kuhusu kushiriki kuwakilisha nchi yako, kuwakilisha bara lako halafu baadae sasa unashindania medali moja. Hiyo ndio maana inaitwa Olimpiki, kuna aina mbalimbali ya watu pale, wawe weupe, weusi kama mimi, lakini tunakimbia kwa pamoja,” alisema.

Aidha, Kipchoge aliwakanusha wale ambao wanasema kuwa amefeli na kumtaka kustaafu akisema kwamba atakuwepo katika mashindano ya Olimpiki Makala ya Los Angeles Marekani mwaka 2028.

Alisema kwamba mtu amefeli ni yule ambaye hajawahi jaribu na kusema kwamba maadamu yeye alijaribu ila akashindwa kumaliza mbio, ina maanisha si mtu aliyefeli.

“Nitakuwa kwenye olimpiki za Los Angeles hata kama ni kwa nia tofauti, mnadhani kwamba mimi nimefeli kwa sababu sikushinda dhahabu katika Paris Olympics? Mtu amefeli ni yule ambaye hajajaribu. Mimi nilijaribu kushinda olimpiki ya 3 lakini haikuwa siku yangu, na hiyo ndio hali ya spoti,” alisema.

Kipchoge kwa mara ya kwanza katika safari yake kwenye marathon, alishindwa kukamilisha kilomita 42 zote za marathon katika mashindano ya olimpiki ya Paris.

Mwaka 2020, alipoteza marathon yake ya kwanza kwa kumaliza katika nafsi ya 8 na mapema mwaka huu wa 2024, Kipchoge alimaliza katika nafasi ya 10 katika marathon ya Tokyo Japani.