Bondia wa Tanzania avuliwa ubingwa wa Afrika

Muhtasari

•Kuvuliwa kwa taji hili kunakuja ikiwa imepita miezi michache tangu avuliwe taji lingine la ubingwa wa mabara la WBF.

Image: TWITTER// MWAKINYO

Bondia wa Tanzania Hassan Hamza maarufu kama Mwakinyo amevuliwa taji lake la ubingwa wa Afrika (African Boxing Union) mara baada ya muda kupita bila kutetea taji hilo.

Kuvuliwa kwa taji hili kunakuja ikiwa imepita miezi michache tangu avuliwe taji lingine la ubingwa wa mabara la WBF.

Mwakinyo alitwaa ubingwa wa Afrika baada ya kumchapa Muangola Maiala Antonio, mwezi mei mwaka jana.

ABU ilimuondoa Mwakinyo kwenye orodha ya mabingwa na kumshusha hadi nafasi ya tatu ya ubora kwenye uzani wa super welter, nafasi ya kwanza ikishikwa na Wale Omotoso kutoka Nigeria, namba mbili ikishikiliwa na Patrick Alotey kutoka Ghana.

ABU pia imeweka wazi nafasi ya ubingwa.

Mwakinyo sasa hana taji la ubingwa analoshikilia. Lakini mbali na kuvuliwa ubingwa huo bado anashikilia nafasi ya 14 duniani kwenye uzito wake wa super welter.