Mandonga Mtu Kazi apigwa marufuku kushiriki mchezo wa ngumi, atakiwa kupima afya

Kamisheni ya kusimamia ndondi za kulipwa Tanzania ilisema ina wasiwasi ha hali yake ya afya kufuatia kipigo cha Moses Golola aliyemshinda kwa Technical Knock Out mwishoni mwa Julai.

Muhtasari

• TPBRC imesema bondia huyo wa ngumi za kulipwa, Karim Mandonga hatoshiriki ngumi mpaka atakapopimwa afya yake.

• Mwishoni mwa mwezi Julai, Radio Jambo iliripoti kwamba Mandonga alipigwa jijini Mwanza na Mganda Moses Golola.

Karim Mandonga
Karim Mandonga
Image: Instagram

Bondia mbwatukaji wa Tanzania Karim Mandonga maarufu Mtu Kazi amefungiwa kujihushisha au kushiriki katika mchezo wa ngumi kwa muda usiojulikana na shirika linalosimamia mchezo huo nchini Tanzania.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Zanziba, ZBC Zanzibar, Kamisheni inayosimamia mchezo wa ngumi za kulipwa nchini Tanzania TPBRC, Mandonga anatakiwa kufanyiwa vipimo vya afya ili kubainishwa kama kweli afya yak iko imara haswa kutokana na kipigo alichopokea mikononi mwa bondia wa Uganda Moses Golola mwezi uliopita.

Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBRC), imemfungia kwa muda Bondia Karim Mandonga kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi wa Afya Muhimbili. TPBRC imesema bondia huyo wa ngumi za kulipwa, Karim Mandonga hatoshiriki ngumi mpaka atakapopimwa afya yake kutokana na kupigwa TKO katika pambano lake na Moses Golola kutoka Uganda lililofanyika Julai 29, 2023 jijini Mwanza,” sehemu ya taarifa hiyo ilisoma.

Mwishoni mwa mwezi Julai, Radio Jambo iliripoti kwamba Mandonga alipigwa jijini Mwanza na Mganda Moses Golola  katika pambano ambalo lilipeperushwa moja kwa moja kwenye runinga ya Azam.

Licha ya kufanya pambano kali, alizidiwa nguvu na Golola, ambaye hatimaye alimtoa katika raundi ya tatu, na kupata ushindi mnono kwenye Technical Knock Out.

Wiki moja tu mapema, Jumamosi, Julai 22, Mandonga alikumbana na misukosuko mingine alipopambana na bondia Mkenya Daniel Wanyonyi.

Hata hivyo, hii ilikuwa kama kulipiza kwa Wanyonyi ambaye alichapwa na bondia huyo mwenye kidomo mnamo Januari mwaka huu katika pambano lililoandaliwa kwenye ukumbi wa kimataifa wa KICC jijini Nairobi.

Baada ya ushindi huo wa Mandonga, alijitapa vikali akirudi nchini kwao na kuzawadiwa gari na mhisani mmoja miongoni mwa zawadi nyingine nyingi.